• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
TAHARIRI: Ushuru zaidi ni mzigo usiofaa

TAHARIRI: Ushuru zaidi ni mzigo usiofaa

KITENGO CHA UHARIRI

HATUA ya mahakama kuu kuharamisha sheria iliyonuia kuanzisha ushuru wa mapato wa asilimia moja ambao ungeshuhudia biashara na kampuni zikitozwa kodi hiyo hata wakati ambapo zimepata hasara, ni jambo la kujivunia.

Hatua hiyo ya mahakama inafaa kuizindua serikali kuhusu mipango yake ya kujiongezea mapato. Si vyema serikali kuongeza pato lake huku biashara hasa ndogondogo ambazo zingeipa hata ushuru zaidi zikianguka.

Je, biashara hizo zikishaanguka, serikali itatoza nani asilimia hiyo ya ushuru?

Naam, hamna serikali yoyote ulimwenguni inayoweza kuhudumu bila kutoza raia wake na mashirika ya kibiashara ushuru maadamu ni kutokana na kodi hiyo ambapo miradi ya maendeleo hufanikishwa mbali na watumishi wa umma kama vile walimu na madaktari kupata mishahara yao.

Ila pia hakuna taifa lililoendelea kiuchumi au kijamii kwa kuwatoza raia wake ushuru wa kupindukia kama huu ambao serikali ya taifa hili imekuwa ikipanga kuanzisha.

Hii ni kwa sababu unapowatoza raia ushuru mwingi, wanakosa uwezo wa kununua bidhaa mbalimbali jinsi ambavyo wangependa na hivyo basi biashara nyingi ambazo huwategemea raia hao kama wateja kukosa mapato.

Katika hali kama hiyo, watu wengi hukosa riziki na shughuli za kiuchumi kupungua, jambo linalodororesha viwango vya maisha.

Cha kusikitisha ni kuwa hata katika hali ambapo ushuru huu vinginevyo ungetumiwa kufadhili, kwa njia ya ruzuku, huduma nyingi za kimsingi, fedha nyingi zinazotokana na ushuru wa mwananchi huliwa kifisadi na Wakenya wachache walio katika nafasi zao.

Katika mataifa mengine ambapo ushuru mwingi hutozwa raia, huduma muhimu kama vile elimu, afya na hata usafiri huwa ni za hali ya juu mbali na kuwa nafuu zaidi.

Tatizo jingine kuu la kutoza ushuru mwingi ni kutoroka kwa wawekezaji wa kigeni ambao huhamia mataifa yaliyo na mazingira bora ya kufanyia biashara.

Kwa ufupi, utozaji ushuru usiokuwa na mipaka una athari nyingi hasi kuliko manufaa hasa kwa mataifa yanayostawi kama vile Kenya.

You can share this post!

Covid-19: Majaribio kufanikisha utoaji chanjo kwa watoto wa...

Mshukiwa wa unajisi aponea kuteketezwa Kambi Moto