• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 3:10 PM
Covid-19: Majaribio kufanikisha utoaji chanjo kwa watoto wa kuanzia umri wa miaka mitano

Covid-19: Majaribio kufanikisha utoaji chanjo kwa watoto wa kuanzia umri wa miaka mitano

Na MARY WANGARI

WATOTO kuanzia umri wa miaka mitano huenda wakaanza kupatiwa chanjo dhidi ya Covid-19 iwapo matokeo ya utafiti uliofanywa na kampuni ya Pfizer yataidhinishwa.

Kampuni ya Pfizer vilevile inasubiri kwa hamu matokeo ya utafiti kuhusu chanjo hiyo uliofanyiwa watoto wachanga wenye umri wa hadi miezi sita, katika hatua ambayo huenda ikavutia hisia kali kutoka kwa jamii ya kimataifa.

Data kutoka kwa majaribio yaliyofanyiwa watoto wasiopungua 2,000 wenye umri kati ya miaka mitano na 11, iliashiria kinga imara ya mwili kutokana na kiwango cha chini cha chanjo hiyo bila athari zozote hasi, kulingana na utafiti huo uliochapishwa Jumatatu, Septemba 20.

Katika utafiti wake, Pfizer ilichunguza kiwango cha chembechembe za damu zinazopigana na ugonjwa huo ili kukadiria uwezo wake wa kutoa kinga ya mwili.

Utafiti huu ulitofautiana na ule wa awali ulioshirikisha watu wazima uliohusisha kulinganisha visa vya virusi vya corona miongoni mwa kundi moja na kundi la watu waliopokea chanjo hiyo.

Licha ya kuwepo kwa visa vya kutosha vya maambukizi miongoni mwa washiriki, Pfizer bado haijatangaza matokeo ya utafiti huo kuhusiana na ufaafu wa chanjo yake, kulingana na msemaji wa kampuni hiyo.

Iwapo itaidhinishwa na serikali ya Amerika ambayo kwa sasa inakagua chanjo hiyo, Pfizer itaweza kuanzisha mchakato wa kusambaza chanjo hiyo kwa watoto mwezi ujao Oktoba huku ikisubiri kibali kutoka kwa Uingereza na Uropa.

“Tuna furaha kujumuisha watoto katika ulinzi unaotolewa na chanjo punde tu tutakapopata kibali hasa tunapochunguza kusambaa kwa virusi aina ya Delta na tishio lake kwa watoto,”

“Visa vya Covid-19 miongoni mwa watoto Amerika vimeongezeka kwa karibu asilimia 240 tangu Julai na kuangazia haja ya utowaji chanjo,” alifafanua mkurugenzi wa Pfizer, Albert Bourla.

Haya yamejiri huku mjadala mkali ukitokota kuhusu kuwapa au kutowapa watoto chanjo ambapo Uingereza tayari imeanza mchakato wa kuwapa chanjo watoto wasio na virusi vya corona wenye umri wa kianzia miaka 12.

You can share this post!

WANGARI: Elimu ya juu iwekeze zaidi katika ujuzi wa...

TAHARIRI: Ushuru zaidi ni mzigo usiofaa