• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 8:03 AM
NGILA: Teknolojia mpya ya mbegu sawa ila wapi hamasisho?

NGILA: Teknolojia mpya ya mbegu sawa ila wapi hamasisho?

Na FAUSTINE NGILA

WIKI iliyopita nilihudhuria uzinduzi wa ripoti kuhusu hali ya kilimo barani Afrika ambapo matokeo ya utafiti kuhusu mbegu yalitolewa.

Habari njema ni kuwa matumizi ya teknolojia yamepelekea kuimarika kwa ubora wa mbegu wanazopanda wakulima wa humu nchini, hali inayochangia kwa juhudi dhidi ya ukosefu wa chakula nchini.

Ripoti hiyo iliyotangazwa na shirika la The African Seed Access Index (TASAI) ilionyesha kuwa visa vya mbegu feki kusambazwa mashambani vimepungua kutoka 36 mwaka wa 2013 hadi 12 mwaka wa 2019.

Pia, ilieleza kuwa jitihada za kampuni za mbegu nchini katika kutokomeza uuzaji wambegu feki umeimarika kutoka asilimia 39 mwaka wa 2013 hadi asilimia 70 mwaka wa 2019.

Lakini ni teknolojia gani hasa, ilitumika kupata matokeo haya?

Kimsingi, wakulima hununua mbegu katika maduka ya kuuza mbegu. Katika karatasi za kupakia mbegu hizo, kuna nambari 12 ambazo zimefichwa kwa stika.

Wakulima hukwaruza stika hizo na kufichua nambari hizo ambazo wanatuma bila malipo kupitia ujumbe mfupi wa SMS na kupokea ujumbe mara moja kuthibitisha kuwa mbegu hizo ni halali.

Kwa mara ya kwanza, nimeona sheria ambazo serikali imeweka kulinda wakulima zikifuatwa.

Katika sheria za kilimo, mbegu zote ambazo zinauzwa kwa mifuko ya chini ya kilo tano inatakiwa kuwa na stika za ithibati.Huu ndio uwezo mkubwa wa teknolojia.

Bila ubunifu huu, mbegu nyingi zinazopandwa Kenya zingetuletea mazao dhaifu tu na kuchangia baa la njaa ambalo hukumba nchi hii kila mwaka.

Hata hivyo, juhudi hizi zinahitaji kupigwa jeki kwani si wakulima wote wanatambua kuwa kuna stika katika mifuko ya mbegu wanayonunua.

Utafiti tofauti uliofanywa na Muungano wa Biashara ya Mbegu nchini (STAK) katika kaunti nane umefichua kuwa kiwango cha wakulima wanaojua kuwa kuna stika hizi ni asilimia 85 kwa wastani.

Hii inamaanisha kuwa asilimia 15 ya wakulima bado wamo katika hatari ya kupanda mbegu feki sababu kuu ikiwa ukosefu wa Habari kuhusu teknolojia hiyo.

Lakini katika utafiti mwingine, licha ya asilimia 85 kutambua stika hizo, ni asilimia 35 pekee kwa wastani ambao wanazikwaruza na kutuma nambari kupitia arafa kuthibitisha ubora wa mbegu.

Yaani, tunajua umuhimu wa teknolojia lakini hatuitumii kutufaa katika njia ambayo inastahili. Sasa basi inakusaidiaje iwapo matapeli watanunua au kuunda stika feki na kupachika kwenye mfuko wa mbegu?

Licha ya kupungua kwa visa vya mbegu feki, bado kuna hatari kuwa ya kuendelea kupata mazao duni hali ambayo katika miaka ya hivi majuzi imekuwa ikipandisha bei ya chakula nchini na kuumiza wananchi ambao tayari wamechoshwa na kupanda kwa gharama ya Maisha kila mwezi.

Ni wajibu sasa wa serikali, kupitia Wizara ya Kilimo, kueneza Habari kuhusu stika hizi katika kaunti zote. Uhamasisho kwa wakulima wadogo na wakubwa ndio utaifaa nchi hii iwapo tunataka kujitegemea katika uzalishaji wa chakula.

You can share this post!

DP yamteua Spika Muturi kuwa mgombeaji urais

Magoha aapa kutetea CBC kwa hali na mali