NA BRIAN OCHARO
MSHUKIWA mmoja ameshtakiwa kwa kumnajisi msichana wa umri wa miaka 13.
Haron Mathenge jana Jumanne alifikishwa mbele ya mahakama ya Mombasa kuhusu makosa hayo.
Kulingana na karatasi ya mashtaka, mshukiwa alimnajisi mtoto huyo katika nyumba moja karibu na soko la Marikiti katika kaunti ndogo ya Mvita.
Katika shtaka la pili, mshukiwa alishtakiwa kwa kufanya kitendo kichafu na mtoto mdogo.
Mathenge alikanusha mashtaka hayo alipofikishwa mbele ya Hakimu Mkuu wa Mombasa, Martha Mutuku.
Upande wa mashtaka unadai kuwa mtuhumiwa alifanya makosa hayo mnamo Aprili 22, 2022.
Hata hivyo mshukiwa huyo ambaye pia anadaiwa kuwa mhubiri aliambia mahakama kuwa mashtaka yamefikishwa dhidi yake kwa nia mbaya.
Mshukiwa huyo aliachiliwa kwa dhamana ya Sh500,000 na mdhamini mmoja wa kiasi sawa na hicho.