Na JOSEPH WANGUI
MAHAKAMA ya Kimataifa kuhusu Uhalifu wa Kibinadamu (ICC) huenda ikafutilia mbali uamuzi wake wa kumwachilia huru kwa dhamana wakili Paul Gicheru kwa kukiuka masharti aliyopewa.
Kulingana na agizo lililotolewa na Jaji Reine Adelaide Sophie Alapini-Gansou, mahakama imefutilia mbali masharti iliyotoa Januari 29, mwaka huu, baada ya Gicheru kujadili na wanahabari kuhusu kesi inayomkabili katika mahakama hiyo iliyoko jijini Hague, Uswisi.
Mahakama ilisema kuwa Bw Gicheru alipowasili nchini Kenya mnamo Februari 1, mwaka huu, alifanya mahojiano Februari 4 na gazeti la humu nchini ambapo alizungumzia kesi inayomkabili.
Jaji Alapini-Gansou alisema kuwa Bw Gicheru alikuwa amepigwa marufuku kuzungumzia kesi hiyo kwenye mitandao ya kijamii na vyombo vya habari.
Jaji alisema kuwa Bw Gicheru alikuwa amefahamishwa masharti yote kabla ya kuachiliwa huru kwa dhamana.
Miongoni mwa adhabu zilizokuwa zimewekwa ni korti kuchukua kabisa Sh1 milioni ambazo Bw Gicheru alitoa kama dhamana na kutolewa kwa amri ya kukamatwa kwake.