ALEX NJERU Na KALUME KAZUNGU
MAMLAKA Huru ya Kuangalia Utendakazi wa Polisi (IPOA) imeanzisha uchunguzi kuhusu vifo tata vya watu wawili katika kaunti za Tharaka Nithi na Lamu.
Katika kaunti ya Tharaka Nithi, IPOA imeanzisha uchukuzi kuhusu kifo cha mwenyekiti wa Muungano wa Kitaifa wa Wahudumu wa Boda Boda, tawi la kaunti hiyo, Willis Mugambi, aliyedaiwa kupigwa risasi na polisi mjini Chuka.
Katika kaunti ya Lamu, mamlaka hiyo inaendesha uchunguzi kuhusu kifo cha mshukiwa mmoja wa ulanguzi wa mihadarati.
Miji Aboud Mohamed, 42, alikamatwa katika mtaa wa Gadeni, kisiwani Lamu akiwa na dawa aina ya heroni. Inadaiwa alimeza dawa hizo ghafla katika harakati za kuficha ushahidi.
Kuhusu mauaji ya Tharaka Nithi, muungano wa wanabodaboda umeonya kuwa utaitisha maandamano ya boda boda kote nchini ikiwa afisa aliyedaiwa kumpiga risasi Mugambi hatakamatwa na kuadhibiwa kwa mujibu wa sheria.
Mugambi 31, ameacha mke na watoto wawili wadogo. Alikuwa ameitwa na polisi kusaidia kutuliza fujo mjini Chuka na ndipo akapigwa risasi na akafa papo hapo.
Muungano wa wanabodaboda unadai kuwa mwendazake alipigwa risasi mara mbili. Hali ya taharuki ingali imetanda katika kaunti ya Tharaka Nithi kufuatia mauaji ya Mugambi.
Mhudumu huyo wa bodaboda alipigwa risasi wakati polisi walikuwa wakiwatawanya waandamanaji ambao waliziba barabara kuu ya Meru-Nairobi wakishinikizi kukamatwa kwa wauaji wa Daniel Mutembei.
Mwendazake ambaye ni mkazi wa kijiji cha Nkwego aliripotiwa kuuawa mwezi Machi na watu watano wanaojulikana na wakazi.
Wakazi wenye hasira, wakiwemo wahudumu wa bodaboda walioziba barabara kwa kutumia mawe na jeneza lililosheheni maiti ya Mutembei wakidai haki. Mugambi alipigwa risasi kifuani na kufa papo hapo mwendo wa saa moja za usiku Jumamosi.
Baadaye makabiliano yalitokea kati ya polisi na wahudumu wa bodaboda huku maiti ya Mugambi ikisalia eneo la tukio hadi usiku.