Na SAMMY WAWERU
SERIKALI za kaunti zimehimizwa kutengea sekta ya kilimo na ufugaji fedha za kutosha ili kuiboresha.
Katibu Mkuu katika Wizara ya Vijana, Bw Charles Sunkuli amesema kuwepo kwa mazao ya kutosha nchini kutaafikika endapo sekta ya kilimo itapata mgao wa kutosha.Chini ya Katiba ya sasa, sekta ya kilimo na ufugaji imegatuliwa, na hii ina maana kuwa utendakazi na huduma zake zipo chini ya serikali za kaunti.
“Ni kaunti chache sana ambazo hupiga jeki ipasavyo kilimo na ufugaji. Ugatuzi unapaswa kuendelezwa ifaavyo,” Bw Sunkuli akaambia Taifa Leo Dijitali, kupitia mahojiano ya kipekee.Huku shirika moja lisilo la kiserikali, Heifer International, likiibua mjadala kuhusu idadi ya chini ya vijana kushiriki kilimo, Bw Sunkuli alisema serikali za kaunti zina mchango mkuu kuhakikisha kilimo kimeboreka.
“Ukosefu wa serikali za kaunti kuimarisha kilimo na ufugaji, utaathiri sekta hii muhimu ambayo sasa i mikononi mwazo,” akasema, akihimiza magavana kuipa kipaumbele katika ugavi wa fedha.Katibu huyu Mkuu pia alisema umewadia wakati maonyesho ya kilimo kutekelezwa mashambani, badala ya mijini ili huduma na mafunzo kufikia wanaolima.
“Mdahalo wetu wa kilimo usakatiwe kule mashinani, ila si mijini. Huko ndiko kilimo na ufugaji kinaendeshwa kwa kiwango kikubwa. Waliokikumbatia wakaribiriwe,” akashauri.