• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:15 PM
Lynn anaamini ipo siku watakubali kazi yake katika uigizaji

Lynn anaamini ipo siku watakubali kazi yake katika uigizaji

Na JOHN KIMWERE 
LYDIA Adhiambo Owino ni miongoni mwa wasanii chipukizi wanaopania kutinga upeo wa kimataifa miaka ijayo katika tasnia ya uigizaji.
Ingawa hajapiga hatua kubwa katika jukwaa la maigizo dada huyu anayefahamika kama Lynn amesema ”Tangia nikiwa mtoto nilitamani kuhitimu pengine kuwa mwimbaji, mwana habari au mwigizaji.
” Hayo tisa. Kumi kando na uigizaji msichana huyu hufanya kazi ya mauzo katika kampuni ya simu ya Safaricom kitengo cha Home Fibre. Binti huyu akiwa mdogo alipenda sana kutazama msanii mcheshi, Vicky Vike maarufu Awinja aliyekuwa akishiriki kipindi cha Papa Shirandula.
Kipindi hicho kilikuwa kinapeperushwa kupitia Citizen TV. Anadokeza kuwa anataka  kujijenga kisanaa akilenga kutinga upeo kimataifa miaka ijayo. Anasema kuwa ana imani kubwa kuwa ndio anaanza kupiga ngoma lakini ipo siku kazi yake itakapokubalika na wanaomchekelea.
”Ninaamini nina kipaji cha kufanya kweli katika masuala ya uigizaji ingawa ninaelewa bayana kuwa shughuli sio mteremko. Ingawa sikufanikiwa kusoma hadi chuo kikuu kama nilivyotarajia niliamua kujiunga na uigizaji pia vichekesho ili kutimiza ndoto yangu,” akasema.
Lydia Adhiambo Owino maarufu Lynn…PICHA/JOHN KIMWERE
Ameshiriki maigizo ndani ya miaka miwili ambapo amefanya kazi na makundi kadhaa ambayo huonesha kazi zao kupitia mtandao wa Youtube ikiwamo Stateman Media, Glighlakes Production  na Love to Laugh Comedy.
Kisura huyo anajivunia kushiriki vipindi mbili vya kuigiza ikiwamo ‘Kortini’  pia ‘Perfect Match’ ambazo hupeperushwa kupitia Ebru TV. Kwa waigizaji wa Afrika Mashariki dada huyu anasema huvutiwa na kazi zake msanii wa Bongo, Wema Sepetu anayejivunia kushiriki filamu kama ‘Kisogo,’ ‘More than a women,’ ‘Heaven sent,’ na ‘Day after a Death,’ kati ya zingine.
Pia hupendezwa na kazi zake mchekeshaji mahiri mzawa wa Uganda, Anne Kansiime. Anaamini kuwa wasanii wa Kenya wakipata ufadhili wanatosha mboga kufanya kazi nzuri na kuvutia wapenzi wa burudani na kugeukia filamu za waigizaji wazalendo.
SERIKALI
Anakariri kwenye juhudi za kuinua uchumi wa taifa hili, serikali inapaswa kutenga fedha kusaidia waigizaji chipukizi maana wakishikwa mkono vizuri wana uwezo wa kuibuka mastaa miaka ijayo. ”Taifa hili limefurika wasanii wengi tu wanaume na wanawake wanaohitaji sapoti ili kukuza vipaji vyao katika tasnia ya maigizo,”
USHAURI
Anashauri wasichana waliopata ujauzito wakiwa na umri mdogo kamwe wasikate tamaa bado wana nafasi ya kujirekebisha na kuishi maisha mema. Anadokeza kuwa pia jamii inapaswa kuwaonesha mapenzi wala sio kuwaponda kama waliokosea.
Anasema hawezi kuweka katika kaburi la sahau akiwa na umri wa miaka 16 alilia sana alipopata ujauzito na mpenzi wake kusepa. Anawataka waigizaji chipukizi hapa nchini waache kubaguana bali waige mtindo wa wenzao katika mataifa yanayoendelea kama Nigeria na Afrika Kusini ambao kila msanii husapoti mwenzie.
  • Tags

You can share this post!

Onkar Rai aibuka mwanamichezo bora Kenya mwezi Juni

Raia wa Nigeria afikishwa Kortini kwa wizi wa muda wa...