• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 5:50 AM
Mahakama yakataa kuagiza kesi dhidi ya Obado ianze upya

Mahakama yakataa kuagiza kesi dhidi ya Obado ianze upya

NA RICHARD MUNGUTI

ALIYEKUWA gavana wa Migori Okoth Obado (pichani) amepata pigo kubwa mahakama ilipokataa kuamuru kesi ya ufisadi wa Sh2.7 bilioni inayomkabili yeye na wanawe ianze upya.

Bw Obado alitaka kesi hiyo ianze upya kufuatia kuteuliwa kwa hakimu aliyekuwa anaisikiza kuteuliwa Jaji wa Mahakama kuu.

Katika uamuzi wake Hakimu mkuu Victior Wakhumile alisema kesi itaendelea mahali ilifikishwa na aliyekuwa hakimu mkuu Lawrence Mugambi ambaye aliteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama kuu.

“Naomba kesi hii ianze kusikilizwa upya baada ya hakimu mkuu Lawrence Mugambi kuteuliwa kuwa Jaji katika Mahakama kuu,” Bw Obado alimsihi hakimu mkuu Victor Wakhumile.

Bw Obado anayeshtakiwa pamoja na watoto wake wanne Dan Achola, Scarlet Susan, Jerry Zachary na Evelyne Odhiambo alisema hawatapata haki kesi hiyo ikiendelea mahala Jaji Mugambi aliiachia.

Washtakiwa wengine Jared Kwaga, mkewe Christine Akinyi, mama yake Penina Auma, ndugu zake Kwaga – Joram Opala na Patroba Ochanda na Carolyne Ochola – wameshtakiwa katika ulaji njama kuipora kaunti ya Migori Sh2.7 milioni.

Mshtakiwa mwingine Scarlet Susan hakufika kortini lakini alifanya kesi hiyo kupitia mtandao.

Upande wa mashtaka utaita mashahidi 59 kuthibitisha jinsi Obado , wanawe na wafanya biashara walivyoichuna kaunti hiyo mabilioni ya pesa.

Inadaiwa Bw Obado alinunua nyumba ya kifahari jijini Nairobi na kutumia pesa za kaunti hiyo kuwalipia wanawe karo wakiendelea na masomo ng’ambo.

Viongozi wa mashtaka walisema ujanja na utumizi mbaya wa mitandao ulitumika kupora kaunti hiyo mamilioni ya pesa.

Bw Obado alishtakiwa 2018 na wakati ugonjwa wa Covid-19 ulipozuka 2020 kesi hiyo haikuendelea kama ilivyopangwa.

Kufikia sasa ni shahidi mmoja tu ameanza kutoa ushahidi.

  • Tags

You can share this post!

Tottenham walaza West Ham United na kuingia ndani ya mduara...

Mwanasiasa ahofia mali yake kupigwa mnada

T L