NA WANGU KANURI
MCHANGIAJI mada kwenye runinga ya Fox News nchini Marekani ametoa kauli yenye utata akidai kuwa wanawake wajawazito nchini Kenya huwa hawaruhusiwi kupiga kura.
Akizungumza katika ukumbi wa mahojiano kwenye stesheni hiyo kutoa hoja kuhusu haki za wanawake katika upigaji kura, Emily Compagno alieleza kuwa katika baadhi ya nchi duniani, wanawake hawana uhuru huo.
“Kwa mfano nchini Kenya wanawake wajawazito hawaruhusiwi kutoka nje ya nyumba kwa hivyo hawawezi hata kupiga kura,” akadai.
Hata hivyo, huu si ukweli kwani kulingana na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) wanawake wajawazito huruhusiwa kupiga kura na hata wanapata afueni ya kutopiga foleni wakati wa kupiga kura.
Kauli yake imewakera Wakenya na watumiaji wa mitandao ya kijamii waliomtaka Compagno aombe msamaha.