NA MERCY MWENDE
MSAIDIZI katika kanisa Katoliki aliyeshtakiwa kwa kumnajisi msichana wa miaka saba amenyimwa dhamana.
Hakimu Mkuu Mwandamizi wa Nyeri, Bi Ruthi Munyi, alisema upande wa mashtaka uliwasilisha sababu za msingi kuruhusu polisi kuendelea kumzuia Michael Muchiri, hadi ipate taarifa za mashahidi na ripoti ya matibabu ya mtoto huyo.
Muchiri, mwenye umri wa miaka 73, anakabiliwa na shtaka la unajisi alilodaiwa kutenda Mei 2023.
Katika uamuzi wake, mahakama pia ilikubaliana na upande wa mashtaka kwamba mtoto huyo yuko hatarini na kuachiliwa kwa mshtakiwa kunaweza kuvuruga upelelezi.
Hakimu Munyi alibainisha kuwa kosa hilo lilifanyika katika kituo kinachosimamiwa na kanisa – ambapo mshukiwa alikabidhiwa malezi ya mtoto.
“Aidha, kosa hilo lilifanyika katika mazingira ambayo watoto wanakusudiwa kuwa salama na kufundishwa nidhamu, ambayo katika muktadha huu ni pamoja na kutii maagizo,” alisema Hakimu Mashauri.
Kesi hiyo itaendelea Oktoba 26, 2023.