• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 12:48 PM
Mwanamke ashtakiwa kuvunja kioo cha gari la Mercedes la mpenzi aliyemtema

Mwanamke ashtakiwa kuvunja kioo cha gari la Mercedes la mpenzi aliyemtema

NA JOSEPH NDUNDA

MWANAMKE mwenye umri wa miaka 23 aliyeshtakiwa kuvunja gari aina ya Mercedes ya aliyekuwa mpenzi wake na kusababisha uharibifu wa Sh207, 000 baada ya kukataa kumruhusu aingie nyumbani amekana mashtaka hayo.

Pamela Macharia anadaiwa kuharibu mali kwa makusudi kinyume na kifungu cha 339 (1) cha Kanuni ya Adhabu baada ya kudaiwa kuvunja gari la afisa wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI).

Hii ni baada ya uhusiano wa kimapenzi kati ya mwanadada huyo na afisa huyo kuisha.

Bi Macharia alishtakiwa kwa kuharibu kimakusudi kioo cha mbele cha thamani ya Sh86,000, kioo cha gari cha thamani ya Sh80, 000, taa ya nyuma Sh25, 000 na kioo cha pembeni cha Sh16, 000 – vyote vikiwa na thamani ya Sh207,000.

Afisa huyo wa polisi anasema alikuwa kwenye nyumba yake wakati ambapo Bi Macharia alibisha mlangoni na alipomfungulia, akakutana naye mlangoni. Anasema alikuwa amekuja bila mwaliko na kwamba alikuwa mlevi.

Afisa huyo akaita walinzi wa makazi hayo ili kumsindikiza nje ya geti mwanadada huyo lakini akakubali kuondoka kwa hiari.

Baadaye polisi huyo alisikia mtu akipiga kitu kama chuma na alipoenda kuangalia alimkuta mwanadada huyo akipiga gari lake na kuliharibu, na hapo ndipo akakimbia kwenda kumzuia.

Alipomuona akimkujia, inadaiwa mrembo huyo alichomoka akitaka kutoroka lakini hapo ndipo alinaswa na walinzi.

Mlalamishi alienda moja kwa moja kuripoti kisa hicho na ndipo mwanadada huyo akakamatwa.

Afisa huyo aliambia wenzake katika kituo cha polisi cha Mowlem kwamba alikuwa ameshatemana na mrembo huyo baada ya kuchumbiana kwa miezi mitatu.

Wawili hao walikuwa wamekutana mtandaoni ambapo afisa huyo alikuwa mteja wake na alikuwa amenunua vitu kadhaa kutoka kwake kabla ya uhusiano wao kuimarika na kuwa wa kimapenzi.

Hata hivyo, Bi Macharia alikanusha mashtaka hayo mbele ya Hakimu Mkuu Mwandamizi Hellen Okwani wa Mahakama ya Makadara na kudai kuwa amekuwa kwenye ndoa na afisa huyo wa DCI kwa zaidi ya miaka mitatu.

Aliambia mahakama kuwa ana ujauzito wa mwezi mmoja wa DCI huyo.

  • Tags

You can share this post!

GWIJI WA WIKI: Abel Nyamari

Rais ahutubu kwa saa moja pekee Raila akisusia hafla bungeni

T L