Na SHABAN MAKOKHA
MWANAMKE mmoja aliyekuwa na umri wa miaka 56 ameuawa kwake nyumbani, Mumias Magharibi kwa kukatwakatwa.
Kulingana na wakazi wa eneo hilo, washukiwa hao walimvamia mwanamke huyo akiwa kwake usiku wa manane mvua ikinyesha. Chifu wa eneo la Lureko, Leo Wanzala, alithibitisha kisa hicho akisema kuwa washukiwa hao walijaribu kubomoa ukuta wa mjane huyo.
“Sababu kuu ya wahalifu hao kubomoa ukuta ilikuwa ni kumfanya mjane huyo afungue mlango,” akasema Bw Wanzala.
Hata hivyo, jirani wanashuku kuwa huenda mjane huyo aliuawa kwa sababu ya mzozo wa shamba.Chifu Wanzala alisema familia hiyo imekuwa na mzozo wa muda mrefu wa shamba ambao ulikuwa bado haujasuluhishwa.
“Mume wa marehemu alikuwa na wake watatu na alinunua shamba hili mwaka wa 2013. Hata hivyo, wanawe marehemu kutoka Mumias Mashariki wamekuwa wakidai mgao wa shamba hilo. Kuna wakati walikuja kugawa shamba hilo ila nikawataka wafuate utaratibu mwafaka,” akasema Bw Wanzala.
Bw Wanzala aliwataka wakazi walio na taarifa zozote kuhusu mauaji ya mjane huyo kufika kwenye kituo cha polisi ili kurahisisha uchunguzi.
Licha ya mwili huo kuchukuliwa na maafisa wa polisi, kamanda wa polisi kaunti ndogo ya Mumias Magharibi Stephen Muoni alisema hajapokea taarifa kuhusiana na mauaji hayo.