• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 1:20 PM
‘Nabii’ kortini kwa madai ya kubaka binti 2 wa mshirika wake

‘Nabii’ kortini kwa madai ya kubaka binti 2 wa mshirika wake

NA JOSEPH OPENDA

MWANAMUME mmoja anayejitambulisha kama nabii, anatarajia kujua hatma yake mwezi ujao, baada ya Mahakama ya Nakuru kumpata na hatia kuhusiana na madai ya kuwabaka binti wawili wa mmoja wa washirika wake.

Mfuasi huyo wa dhehebu la Legio Maria, mwenye umri wa miaka 66, amekuwa akidai kuwa kipofu mwenye macho ya kiroho yanayomwezesha kuponya matatizo kwenye viungo vya uzazi kwa wanawake.

Alishtakiwa baada ya kukaa kwa mshirika wake kwa muda wa wiki moja ingawa alikanusha tuhuma hizo.

Mnamo Mei 8, korti ilitoa uamuzi kwamba mshukiwa ana kesi ya kujibu. Akijitetea mnamo Mei 15, mshukiwa alikanusha mashtaka akidai anasingiziwa.

Alieleza mahakama alialikwa na mwanamke huyo awaombee watoto wake akisema ni mtumishi aliye na uwezo wa kuwaombea na kuwaponya watu.

Hakimu Mkazi, Bw Edward Oboge atatoa uamuzi mnamo Juni 6. Inadaiwa kuwa masaibu yake yalianza mnamo Januari 1, 2023, alipozuru makao ya mshirika wake mjini Njoro kwa shughuli ya maombi.

Mama huyo aliyekuwa akiishi na binti zake wawili, alimkaribisha mwanamume huyo na kukubali kumpa makao kwa muda, kabla ya mshukiwa kuwabaka wanawe mnamo Januari 5, 2023.

Kulingana na nakala ya mashtaka, Bw Wekesa alishtakiwa kuwa mnamo Januari 5, 2023, katika eneo la Golf Estate mjini Njoro, alijamiiana kimaksudi na wanawake hao bila idhini kutoka kwao, mashtaka aliyokanusha.

Mhasiriwa mmoja aliyetoa ushahidi kortini, alisema mama yao alimpokea mwanamume huyo aliyedai kuwa kipofu na nabii wa Legio Maria, na kumpa chumba kilichokuwa karibu na nyumba yao.

Siku ya tukio hilo, mwanamume huyo alimwita chumbani kwake na kumwambia angeweza kuona kupitia macho yake ya kiroho kuwa ana tatizo la utasa na angeweza kumponya.

Mwanamke huyo alisema, alinaswa kirahisi na mwanamume huyo kwa sababu ya uvimbe kwenye kiuno chake ambao alihofia ungemfanya kuwa tasa.

“Ilikuwa mwendo wa saa tano usiku aliniambia nizime taa, nivue nguo na niingie kitandani ili akande uvimbe kwenye kiuno changu huku akinikumbusha kwamba huenda nisipate mtoto,” alisema mwanamke huyo.

“Alinivuta karibu na kabla nijue kilichokuwa kikiendelea tulikuwa tunashiriki ngono. Nilipojaribu kupiga mayowe alinionya nikifanya hivyo au kumwambia mtu yeyote ningejionea mwenyewe kitakachotendeka. Aliniambia pia amefanya hivyo na wanawake wengine,” alisema.

Baada ya tukio hilo, mshukiwa alimweleza avae nguo na kuondoka.

Hata hivyo, alistaajabu alipokwenda chumbani kwake na kumpata dada yake akilia na alipomuuliza akamwambia mshukiwa alikuwa amemtendea vivyo hivyo.

  • Tags

You can share this post!

Obiri kutetea taji la Great Manchester Run mnamo Mei 21

Mahasla kunywa chai bila sukari

T L