• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:15 PM
Rais Kenyatta azindua kiwanda cha kutengeneza silaha za idara ya usalama Ruiru

Rais Kenyatta azindua kiwanda cha kutengeneza silaha za idara ya usalama Ruiru

Na SAMMY WAWERU

RAIS Uhuru Kenyatta, Alhamisi amezindua kiwanda kidogo cha kutengeneza silaha zitakazotumika na maafisa wa usalama nchini.

Kiwanda hicho kimezinduliwa eneo la Ruiru, Kaunti ya Kiambu, Rais Kenyatta akisema hatua hiyo itasaidia kuimarisha hali ya usalama nchini.

“Uzinduzi wa kiwanda hiki unaashiria Kenya itaweza kujisimamia na kujitegemea kutengeneza silaha zitakazosaidia kuimarisha usalama nchini,”akasema kiongozi huyo wa nchi.

Alisema kuzinduliwa kwa kiwanda hicho kunaenda sambamba na mikakati yake katika Ajenda Nne Kuu.

Aidha, Rais Kenyatta alisema mradi huo utasaidia kubuni nafasi za kazi kwa vijana, kupitia wafanyakazi watakaoajiriwa.

“Ni fahari kufungua kiwanda hiki kidogo cha uundaji wa silaha. Hatua hii inaenda sambamba na mikakati iliyoko katika Ajenda Nne Kuu, nafasi za ajira kwa vijana wetu zitapatikana. Isitoshe, ni miongoni mwa malengo tunayopania kuafikia kama taifa kwenye Ruwaza ya 2030,” akasema.

Uzinduzi wa kiwanda hicho unatazamiwa kusaidia kuondoa mawakala wenye tamaa za ubinafsi katika uagizaji wa silaha za idara ya usalama kutoka nje ya nchi, na ambao wametajwa kupunja serikali.

“Safari tuliyoanza leo si rahisi, itahitaji kujitolea, kuwekeza kupitia fedha na nguvukazi, na pia mafunzo kwa watakaosaidia kuifanikisha,” akasema.

Waziri wa Usalama wa Ndani, Dkt Fred Matiang’i, Mkuu wa Majeshi Kenya (KDF), Meja Jenerali Robert Kibochi, na vigogo wengine wakuu katika idara ya usalama nchini walihudhuria uzinduzi huo.

“Hii ni hatua kubwa tumepiga mbele na kimaendeleo kama taifa, kusaidia kuimarisha hali ya usalama,” akasema Dkt Matiang’i.

You can share this post!

AKILIMALI: Ujuzi wa kuchonga vinyago unampa tabasamu kila...

AKILIMALI: Asihi wakulima kukumbatia kilimo kidijitali