NA FAITH NYAMAI
RAIS William Ruto jana Ijumaa aliteua jopo la wasomi zaidi ya 40 kuangazia upya utekelezaji wa Mtaala wa Umilisi na Utendaji (CBC), elimu ya kimsingi, kiufundi na chuo kikuu.
Jopo hilo litaongozwa na Prof Raphael Munavu na limepewa muda wa miezi sita kumaliza kazi yake. Pia litakuwa likimwaarifu Rais Ruto kila baada ya miezi miwili.
“Wanachama wa jopo hilo watapokea maoni kutoka kwa wadau na umma kupitia mikutano. Litaendesha majukumu yake kwa kuzingatia kanuni zilizowekwa,” akasema Rais Ruto.Kati ya wanachama wa jopo hilo ni Prof David Som, Dkt Halima Saado, Kasisi Seline Chepngeno, Prof Hassan Mwakimako, Collins Odote na Bernard Kariuki.
Pia Rais Ruto aliteua makatibu saba wa jopo hilo ambao ni Dkt Elyas Addi, Patita Tingoi, Dkt David Njegere , Prof Jackson Too, Dkt Reuben Nthamburi Mugwuku, Richard Miano na Eunice Gachoka.
“Jopo hili litajikita katika kutoa mapendekezo ya kuboresha elimu ya chekechea, kuangazia majukumu ya wazazi na kushirikishwa katika shughuli za elimu. Pia litaangazia masuala yanayohusisha walimu na mwongozo ambao utaamua jinsi utekelezaji wa mtaala huu utakavyouwanufaisha wanafunzi,” ikasema notisi ya gazeti.
Dkt Ruto ameamrisha jopo hilo liangazie pia sheria zinazoongoza utendakazi wa Bodi ya Elimu ya Juu (HELB), Vyuo vya Kiufundi (TVET) na taasisi mbalimbali za masomo.
Subscribe our newsletter to stay updated