• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:50 AM
Ruto atumia ‘BBI’ aliyoikataa kutunuku wandani

Ruto atumia ‘BBI’ aliyoikataa kutunuku wandani

NA ONYANGO K’ONYANGO

RAIS William Ruto ametumia pendekezo lililokuwa katika Mpango wa Maridhiano (BBI) alioupinga ili kutimiza ahadi alizotoa kwa washirika wake wakati wa kampeni za kabla ya uchaguzi mkuu wa Agosti 9.

Rais Ruto amebuni wadhifa wa waziri mwenye mamlaka makubwa ambao utashikiliwa na kiongozi wa ANC Musalia Mudavadi.

Wadhifa huo unalinganishwa na ule wa waziri mkuu uliokuwa katika BBI alioupinga, na kuangushwa na Mahakama ya Juu.

“Atakuwa akisaidia Rais na Naibu Rais kusimamia wizara za serikali na idara mbalimbali. Pia atakuwa akisimamia miradi ya serikali na utekelezaji wake pamoja na majukumu mengine ambayo anaweza kupokezwa na Rais,” akasema Dkt Ruto alipomteua Bw Mudavadi kwenye wadhifa huo.

Bw Mudavadi aliwahi kupinga nafasi hiyo kwenye BBI.

Bw Mudavadi alisema waziri mkuu anastahili kuteuliwa kutoka kwa chama anachotoka Rais.

Kando na kumpa Bw Gachagua wadhifa wa Naibu Rais, Dkt Ruto ametimiza ahadi alizotoa kwa wakazi wa Mlima Kenya kwa kuwapa nafasi saba za uwaziri pamoja na nyadhifa nyingine.

Maeneo ya Mlima Kenya na Bonde la Ufa ndiko Dkt Ruto alipata uungwaji mkono mkubwa na kuchangia ushindi wake wa wadhifa wa Urais.

“Rais wetu si kiongozi binafsi na hana kisasi na wale ambao walimpinga. Lengo lake ni kuwajumuisha Wakenya wote katika serikali yake na nina imani ataongoza nchi hii vizuri,” akasema Mwenyekiti wa UDA Johnstone Muthama.

Alipokuwa akitangaza baraza lake la mawaziri, Dkt Ruto alisema kuwa aliamua kuwatunuku wandani wake nyadhifa mbalimbali serikalini kwa sababu, waliamua kufanya kazi naye na kuchangia ushindi wake wakati baadhi yao walikuwa wakiandamwa na utawala uliopita.

Kando na Mabw Rigathi na Gachagua, wengine ambao Dkt Ruto aliwatimizia ahadi ni Moses Wetang’ula na Amason Kingi waliopata nyadhifa za uspika kwenye seneti na bunge la kitaifa kutokana na ushirikiano wa wabunge na maseneta wa Kenya Kwanza.

  • Tags

You can share this post!

Ulinzi Starlets yamsajili straika matata Joy KingLady Oriyo

Ruto aunda jopokazi la wasomi kuchunguza CBC

T L