Na WANDERI KAMAU
MWAKILISHI wa Kike wa Kaunti ya Murang’a, Bi Sabina Chege, jana Jumanne alikosa kuhudhuria kikao ambapo alitarajiwa kuhojiwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kuhusiana na matamshi aliyotoa kuhusu wizi wa kura.
Bi Chege alitoa matamshi hayo kwenye mkutano wa kisiasa wa vuguvugu la Azimio la Umoja katika Kaunti ya Vihiga wiki iliyopita, ambapo alidai kuwa Chama cha Jubilee kilishiriki wizi wa kura 2017.
Kupitia mawakili James Orengo, Otiende Amollo na Martin Oloo, mbunge huyo alisema hangeweza kufika kwenye kikao hicho kwani anaugua na amelazwa katika Nairobi Hospital kupokea matibabu.
Kesi dhidi yake ilipangiwa kufanyika jana mbele ya Kamati Maalum ya Tume Kuhakikisha Sheria za Uchaguzi zinazingatiwa.
Bw Amollo aliwasilisha barua kutoka kwa Dkt Eric Munene kuthibitisha mteja wake ni mgonjwa.
“Tunaiomba tume kuahirisha kikao cha kesi hii hadi pale mteja wetu atakaporuhusiwa kutoka hospitalini,” akasema.