NA MERCY KOSKEI
MWANAKONTETI kwa Esther Muthoni almaarufu Nairofey, amesema kuwa analenga kuishi na mumewe Duncan Macharia almaarufu Yeforian kama mke na mume licha ya changamoto za hivi majuzi.
Nairofey alisema kuwa wanajitahidi sana kutimiza lengo hilo kama wapenzi licha ya kukashifiwa mitandaoni.
“Kwa kila mume na mke walio kwenye mahusiano ya mbali bila shaka hilo ndilo lengo kuu. Tunapanga mipango kutimiza hilo. Hivi karibuni tutakuwa tunaishi pamoja na nina furaha sana. Namuomba Mungu afanikishe maana ni moja ya malengo yangu kuu kwa sasa. Kuishi na mume wangu kabisa,” alisema
Mnamo 2022, wapenzi hao walifunga ndoa lakini walikumbwa na changamoto kwenye mitandao ya kijamii.
Hata hivyo, walirudiana mwaka huu na kushangaza wengi jambo ambalo lilimpelekea rafiki yake wa karibu, Shorn Arwa, kueleza shaka yake kuhusu uamuzi wake wa kurudiana tena na Yeforian.
Kujibu maoni ya Shorn na wanamitandao, Nairofey alichapisha video kwenye mtandao wake wa YouTube Oktoba 11, 2023, akisisitiza umuhimu wa kutozingatia wapinzani.
Alisema kuwa nguvu ya kweli inatokana na kupuuza wambea na kutokuwa na hitaji la kujithibitisha kwa wengine.
Kuhusu kukuza familia yao, Nairofey alifichua kuwa hajawahi kutumia madawa ya kupanga uzazi hapo awali na kuwa ana matumaini kwamba atapata mimba kwa urahisi wakati ufaao.
“Sijawahi kutumia vidhibiti mimba. Sijisumbui na hofu ya kupata mimba kwa sababu niko kwenye uhusiano wa mbali. Ninamuona mume wangu kwa muda mfupi na tuna njia zetu za kufanya mambo,” aliongeza.
Mwanzoni mwa mwaka, wapenzi hao walitengana na kutangaza tofauti zao kwenye mitandao ya kijamii.
Kulingana na Yeforian, alihusika na uboreshaji wa maisha ya Nairofey na pia alimshutumu kutoka nje ya ndoa.
Nairofey, kwa upande wake, alisema kuwa Yeforian alimhada kusaini mokataba ambayo ingepelekea kupoteza mapato yake endapo wangekatiza uhusiano wao.