KUNDI moja la kutetea haki za kibinadamu limetetea watu 1,786 waliotajwa na serikali ya kaunti ya Homa Bay kama wafanyakazi ghushi na wakasimamishwa kazi Agosti mwaka huu.
Wanaharakati hao wa haki wameitaka serikali ya Gavana Gladys Wanga kutoa kwa umma ripoti ya shughuli ya ukaguzi wa wafanyakazi iliyogundua kuwa serikali hiyo hutumia Sh300 milioni kila mwaka kulipa wafanyakazi ambao hawakuajiriwa kisheria.
Bw Evance Oloo, mwenyekiti wa kundi la Interface Community Help Desk, jana alisema kutolewa kwa ripoti hiyo kwa umma ndio ya kipekee itakayowawezesha waathiriwa hao 1,786 watajua sababu zilizochangia wao kusimamishwa kazi.
Ripoti iliandaliwa na kampuni ya PriceWaterhouse Coopers (PWC) iliyoendesha ukaguzi wa wafanyakazi ilifichua kuwa serikali ya kaunti ya Homa Bay ilikuwa ikiwalipa mishahara wafanyakazi ambao hawakuelewa majukumu yao.
Aidha, wengine wao hawakuwajua wasimamizi wao na wenzao kazini.
Isitoshe, iligunduliwa kuwa baadhi ya wafanyakazi hao walitumia vyeti feki vya masomo kupata nafasi hizo.
Zaidi ya hayo ilifichuka kuwa serikali ya gavana Wanga ilikuwa ikiwalipa mishahara watu 129 ilhali maelezo yao hayakuwa katika sajili rasmi ya wafanyakazi wa kaunti hiyo.
Baada ya ripoti ya ukaguzi huo kuwasilishwa kwa serikali ya kaunti ya Homa Bay, baadhi ya wafanyakazi waathiriwa walipewa barua za kuwatema. Wengine wao wamekuwa wakifika kazini kila siku lakini hawapokei mishahara yao kila mwezi.