Na MWANDISHI WETU
Huku idadi ya watu ikiendelea kuongezeka na wengine wakihamia mijini, uchafu unaotokana na plastiki unazidi kuwa tishio kwa afya ya umma sio tu hapa Kenya, bali ulimwenguni kote.
Kulingana na ripoti ya Mpango wa Mazingira wa Umoja wa Mataifa UNEP (2018), inakadiriwa kwamba tani 2,400 za taka huzalishwa kila siku jijini Nairobi, ambapo asilimia 20% ni uchafu wa plastiki.Aidha, udhibiti duni wa taka pamoja na shinikizo la kuhamia jijini ni baadhi ya masuala ambayo yamechangia kuendelea kwa tatizo hili.
Duniani kote, chupa milioni moja za maji ya kunywa za plastiki hununuliwa kila dakika, huku mifuko ya plastiki trilioni 5 ya kutumika mara moja ikitumika kila siku. Kwa ufupi, nusu ya plastiki zote zinazozalishwa, zimesanifiwa kutumika mara moja pekee.
Inasemekana kwamba ulimwenguni kote, plastiki tani milioni 300 huzalishwa kila siku, uzani ambao ni sawa na ule wa idadi yote ya watu ulimwenguni.Watafiti wanakadiria kwamba zaidi ya tani bilioni 8.3 za plastiki zimezalishwatangu miaka ya hamsini na takriban 60% ya plastiki hizo zimeishia katika ardhi na majini.Aidha, ni 9% pekee ya taka za plastiki zinazozalishwa ambazo huundwa upya na takriban 12% zikibadilishwa, huku zilizosalia 79% zikiwa ardhini na majini.
Tani milioni 8 za plastiki huishia baharini ambapo nyingi yazo hubebwa kutoka mitoni. Uchafu huu wa plastiki mitoni umehusishwa na hatari nyingi ikiwa ni pamoja na ongezeko la maradhi na uchafuzi wa mazingira.Ripoti ya mwaka jana ya kamati ya kitaifa kuhusiana na malalamishi ya kimazingira NECC, ilionyesha kwamba Kenya hupoteza wastani wa $27 milioni, kwa kutibu maradhi yanayohusiana na udhibiti duni wa taka.
Lakini hata mambo yanavyozidi kuonekana kuwa mabaya, kuna matumaini. Mojawapo ya mashirika ambayo yamekuwa mstari wa mbele katika kukabiliana na tatizo la taka za plastiki nchini ni Chemolex Company Limited.Kampuni hii imezindua mfumo maalum wa kunasa uchafu wa plastiki na kuubadilisha kuwa nyenzo za ujenzi kama vile fito, vigae vya kuezeka paa na vibao vya kuunda fanicha.
Mfumo huu unahusisha mtambo maalum wa kunasa uchafu wa plastiki unaoelea mitoni.“Kwa kawaida mtambo huu unaingizwa mtoni katika maeneo hususan kisha hunasa uchafu huu. Kwa upande wetu, tumeweka mitambo hii katika mito Athi na Nairobi kwani kulingana na taasisi ya utafiti wa baharini nchini (Kenya marine research institute), asilimia 60 ya uchafu wa plastiki unaopatikana Bahari Hindi unatoka katika mito hii,” aeleza Clifford Okoth Owino, mwanzilishi mshirika wa Chemolex Company Limited.
Baada ya kukusanywa, uchafu huu, hutengwa kuambatana na aina tofauti, kusagwa kisha kusafirishwa hadi katika viwanda vya shirika hili jijini Nairobi na Athi River, ambapo shughuli ya uundaji bidhaa hizi upya huanza.“Kwa upande wetu, tunahusika na uundaji upya wa aina 26 za plastiki ikiwa ni pamoja na Low-density polyethylene (LDPE), Polyethylene terephthalate-PET, inayotumika kuunda chupa za maji, na Styrofoam aina ya plastiki inayotumika kuunda vifaa vya kupakia vyakula na bidhaa za eletroniki,” aeleza Bw Okoth.
Hii ni teknolojia mpya hapa nchini ambapo kulingana na Bw Okoth, waliwasilisha bechi ya kwanza ya bidhaa walizounda kwa taasisi ya utafiti na ustawi wa viwanda nchini-KIRDI, na wanasubiri matokeo ya majaribio kadha wa kadha ya usalama, kabla ya kupata idhini ya kuanza matumizi ya bidhaa hizi.“Tayari tunatarajia kupokea hati hivi karibuni na hata mipango ipo ya kuanza kutumia baadhi ya matofali haya kuunda vijia vya wapita njia hapa mtaani Kariobangi,” aeleza Bw Okoth.
Mbali na kuimarisha mazingira, vilevile kuzuia madhara ya kiafya ya baadaye, shirika hili limekuwa likihamasisha umma kuhusu umuhimu wa kudhibiti taka na kushughulikia mazingira, mafunzo ambayo huendelezwa hasa shuleni na katika taasisi zingine za masomo ya juu.
Bila shaka hii ni habari njema katika enzi hizi ambapo ulimwengu unaendelea kuzama kutokana na ongezeko la taka za plastiki ambazo zimeendelea kusakama mito, maziwa na bahari.Lakini licha ya habari hii njema, kuna mengi yanayostahili kufanyika ili kuhakikisha kwamba ulimwengu na hasa Kenya inatimiza ndoto yake ya kukabiliana na janga hili la plastiki.
Kwa mfano, Kenya bado ingali nyuma katika harakati za kufanikisha mfumo thabiti wa uundaji upya taka na hasa za plastiki. Ni suala ambalo hudhihirika hasa mvua inaponyesha na kusababisha mafuriko yanayotokana na mitaro kuziba kutokana na uchafu wa plastiki.Viwanda vya kuunda upya bidhaa kutokana na uchafu wa plastiki bado vinakumbwa na changamoto ya kuendeleza shughuli zao, huku ufadhili ukiwa tatizo kuu.
“Kwa mfano, ili kupata muundo msingi wa kiwanda sawa na hiki, inachukua takriban Sh20 milioni, kiasi ambacho sio kila mmoja anaweza kumudu,” aeleza Bw Okoth.Pia, ukosefu wa mitambo muhimu kama vile mashine ya kusaga plastiki, umekuwa tishio kubwa.
“Mitambo ya kusaga plastiki inayopatikana hapa nchini ni ile ya kusaga aina moja ya plastiki, ilhali kwa mfano kiwanda kama chetu kinahusika na aina nyingi za plastiki,” aeleza.Mbali na hayo, kuna tatizo la muda mrefu unaotumika katika majaribio ya bidhaa zinazoundwa kwa njia hii.
“Hii ni teknolojia mpya ambapo lazima kuwe na majaribio mengi kuhakikisha kwamba bidhaa za ujenzi tunazounda, ni salama. Kwa mfano, shirika hili liianzishwa mwaka wa 2017 ilhali ni mwaka jana tu tulipowasilisha bechi ya kwanza ya bidhaa tulizounda kwa KIRDI,” aeleza.Lakini tatizo kuu ni la kimfumo.
Kwa mfano, hapa nchini hakuna mfumo maalum wa uundaji bidhaa mpya kutokana na taka huku mzigo wa kuunda upya bidhaa kutokana na taka za plastiki ukiachiwa raia wa kawaida ambao hawawezi stahimili kiwango kikubwa cha uchafu wa plastiki unaozalishwa humu nchini.
Mwaka jana, mkurugenzi wa idara ya utiifu na utekelezaji sheria ya Halmashauri ya Kitaifa ya Kudhibiti Mazingira NEMA, Zephaniah Ouma, aliliambia shirika la habari la kimataifa la Al Jazeera kwamba Kenya huunda upya asilimia 15 pekee ya uchafu wa plastiki inayozalisha.Hiki ni kiwango kidogo sana na huenda kikarejesha nyuma ratiba ya Kenya ya kufikia asilimia 80 ya uundaji upya bidhaa kutokana na uchafu wa plastiki kufikia mwaka wa 2030.