• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 10:08 PM
Wazee wa Kaya watishia kulaani waliosingizia Naibu Gavana

Wazee wa Kaya watishia kulaani waliosingizia Naibu Gavana

Na CHARLES LWANGA

WAZEE wa Kaya wamewataka wale waliosingizia Naibu Gavana wa Kilifi, Bw Gideon Saburi mashtaka ya kupotosha wakati wa janga la Corona wamuombe msamaha la sivyo wawalaani.

Wakizungumza na wanahabari baada ya kufanya maombi ya shukrani eneo la Rabai kaunti ya Kilifi, baada ya Bw Saburi kuondolewa shtaka la kuambukiza umma virusi vya corona kiholela, wazee hao kutoka Kaya zote tisa za jamii ya Mijikenda pia waliitaka serikali imfidie Bw Saburi kwa kumtesa kimawazo.

Wakiongozwa na Mzee Stanley Kenga kutoka Kaya Ribe, waliwataka wote waliohusika katika uchochezi uliosababisha kushtakiwa kwa naibu gavana huyo, waombe msamaha.

“Bw Saburi ni mwana wetu na anafaa kuheshimiwa. Wale wote waliohusika katika madai ya urongo kuhusiana na naibu gavana wamuombe msamaha. Wasimpige vita mtoto huyu. La sivyo kutoka mchangani hadi mbinguni walaaniwe,” akasema.

Mzee Erastus Kubo alisema Bw Saburi ameteseka kisaikolojia na kiafya, na serikali inafaa imlipe fidia kutokana na masaibu aliyoyapitia yasiyo na ukweli wowote.

“Kwa sababu kesi hiyo imeisha, tunawataka wale wote waliomletea masaibu hayo wamuombe msamaha,” akasema.

Kwa upande wake, Bw Tsuma Nzai, ambaye ni mratibu wa baraza la wazee wa Kaya, alisema baadhi ya wale ambao wanafaa kuomba msamaha ni wafanyikazi wa Kaunti ya Kilifi, ambao walichapisha filamu na hadithi za uongo mitandaoni, wakimkashifu Bw Saburi kwa kuambukiza watu virusi vya Corona akijua alikuwa na virusi.

“Kuna filamu ambazo zilivuma katika mitandao ya kijamii. Baadhi ya wakazi wakiwemo viongozi walimkashifu Bw Saburi na kumwita hayawani anayefaa kufungwa au hata kupigwa mawe. Hao ndio baadhi ya watu wanaofaa kuomba msamaha,” akasema.

Alhamisi iliyopita, mahakama ya Mombasa ilimwondolea Bw Saburi shtaka hilo la kukusudia kuambukiza watu Corona.Baada ya kutoka mahakamani, Bw Saburi alihutubia wanahabari na kusema amewasemehe wale waliomchafulia jina.

Lakini Gavana Amason Kingi akiongea na Taifa Leo kwa simu, alikanusha kupokea ripoti za wakora katika serikali yake. Alimshauri naibu wake awasilishe malamishi hayo mbele ya Tume ya Kupambana na Ufisadi (EACC), Mkurugenzi wa Ujasusi (DCI) na idhara nyingine za serikali za kukabiliana na maovu.

You can share this post!

China kuchanganya chanjo mbalimbali kukabili corona

Kocha Ouma apigwa kalamu, FKF yaajiri More kung’oa...