• Nairobi
  • Last Updated May 16th, 2024 8:50 PM
IPOA inajikokota kuchunguza polisi walioua raia – Familia

IPOA inajikokota kuchunguza polisi walioua raia – Familia

NA KALUME KAZUNGU

FAMILIA zilizopoteza wapendwa wao katika hali tatanishi wakiwa mikononi mwa polisi zinalaumu Mamlaka ya Huduma na Utendakazi wa Polisi (IPOA) kwa kukosa kuwajibikia haki kwa waliodhulumiwa.

Wakizungumza na Taifa Leo mjini Lamu, ndugu, dada, wazazi na marafiki wa waliouawa walieleza kushangazwa kwao na jinsi IPOA inavyoendelea ‘kujikokota’ katika kutafiti na kuwachukulia hatua maafisa waliochangia maafa kwa wapendewa wao.

Familia hizo zinalalamika kuwa miezi kadhaa imepita tangu walipopatwa na mikasa ya watu wao kuuawa na polisi ilhali IPOA ikikosa kuwafikia na kuwaeleza hatua zilizopigwa katika kuchunguza dhuluma hizo.

Feiswal Miji, ambaye ni nduguye Aboud Miji Zambavu anayedaiwa kuuawa kwa kunyongwa na polisi waliomlazimisha kutapika dawa alizokuwa anadaiwa kumeza mnamo Aprili 2023, alisema licha ya mwenyekiti wa IPOA Anne Makori kufika Lamu na kuwaahidi kwamba wangepata haki ya mpendwa wao, kufikia sasa hakuna lolote ambalo wamefahamishwa.

Bw Miji aliitaja IPOA kuwa kitengo kinachotumiwa vibaya kunyamazisha waliodhulumiwa kupitia matamshi matamu ilhali hakuna vitendo vyovyote.

“Walisema wanachunguza tukio la mauaji ya ndugu yangu yaliyotekelezwa na polisi na kwamba wangetoa ripoti yao na kuhakikisha washukiwa wanachukuliwa hatua kali za kisheria katika kipindi cha wiki mbili pekee. Twashangaa tuko mwezi wa Julai sasa. Karibu miezi minne imepita na hakuna lolote limefanywa ili kakangu kupata haki. Nahisi hii IPOA ni kitengo kilichoundwa tu ili watu wajiajiri na kula pesa bwerere. Sina imani na IPOA,” akasema Bw Miji.

Familia nyingine inayolalamikia utepetevu wa IPOA ni ile ya mama Mariam Mohammed Hilesi ambaye pia alimpoteza kijana wake Omar Hussein Shizo mapema Aprili 2023.

Omar alipatikana akiwa ameuawa nje ya kambi ya polisi wa BPU eneo la Kiangwe msituni Boni muda mfupi baada ya kufikishwa kambini humo kwa madai ya kuiba kilo 5 za chakula cha msaada.

Bi Hilesi alisema licha ya IPOA kuahidi kuchunguza tukio hilo na wahusika kuadhibiwa, hakuna hatua yoyote kufikia sasa wamejulishwa kwamba imechukuliwa na haki kutendeka kwa familia yake.

“Walikuja tu na kutuahidi wanachunguza. Tangu hiyo Aprili, 2023 hadi sasa sijapigiwa simu kufahamishwa hatua zilizoafikiwa hadi sasa. Wamenyamazia tu ilhali mimi nikiendelea kuumia. Ninaamini walinda usalama walihusika na kifo cha mwanangu na ni wajibu wao IPOA kututafutia haki kama familia,” akasema Bi Hilesi.

Mjini Hindi, familia ya mwanafunzi wa Kidato cha Tatu Mohamed Shee Omar pia imesalia bila jawabu tangu kijana wao alipopigwa risasi na kuuawa na polisi usiku wa Juni 17, 2023.

Binamu wa mwendazake, Bi Baraka Athman anasema wamekuwa wakisubiri kutimizwa kwa ahadi ya IPOA kuchunguza na kuwachukulia hatua walinda usalama waliohusika na mauaji tata ya kakake.

“Walisema tutulie na baada ya kipindi cha wiki mbili pekee watakuwa wametoa ripoti na wahusika waadhibiwe. Hatujajulishwa hatua zozote zilizopigwa kufikia sasa. Bado tuko gizani,” akasema Bi Athman.

Hali ni ile ile kwa familia ya Mgana Mseja,46, ambaye inadaiwa alipatikana amejitia kitanzi ndani ya seli ya kituo cha Polisi cha Mokowe, Kaunti ya Lamu mnamo Mei 2023.

Familia pia ilikuwa imeahidiwa na IPOA kwamba uchunguzi ungefanyika haraka na kubaini iwapo polisi walihusika kwa njia yoyote na kifo cha Mseja.

Hadi sasa hakuna hatua zozote walizofahamishwa kuhusiana na tukio hilo.

Afisa Mshirikishi wa Shirika la Kutetea haki za Binadamu la MUHURI, kaunti ya Lamu, Mohamed Skanda aliisisitizia IPOA kuwajibikia jukumu lao kwa kuhakikisha waliokiuka haki za binadamu, hasa polisi, wanachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

“Siridhishwi na kucheleweshwa kwa uchunguzi kuhusiana na maafa yanayohusishwa na polisi hapa Lamu. Familia hazijui ziende wapi, licha ya IPOA kuzipa matumaini kwamba haki ingetendeka kwao. Twataka mabadiliko kwa IPOA,” akasema Bw Skanda.

Katika mahojiano na Taifa Leo aidha, Mkurugenzi wa IPOA Ukanda wa Pwani, Hussein Aden, alikana madai kuwa IPOA haiwajibikii kazi yake.

Badala yake, Bw Aden aliwataka wananchi kuzidisha imani yao kwa IPOA, akishikilia kuwa afisa yeyote wa usalama aliyekaidi amri kazini lazima aadhibiwe.

“Watu wasiseme tumefeli majukumu yetu. Kwanza, nataka familia za Lamu kutambua kuwa tumepiga hatua kubwa katika kuchunguza visa vinavyohusishwa na polisi eneo hilo. Wawe wavumilivu kwani shughuli ya kuandaa ripoti za uchunguzi lazima  itekelezwe kwa umakinifu mkuu. Tuko imara na wazidi kuwa na imani na sisi,” akasema Bw Aden.

  • Tags

You can share this post!

Upanzi wa mikoko waleta afueni kwa wakazi wa Mkupe

Kizaazaa demu akimpokonya polisi bunduki ndani ya...

T L