Na KNA
WAKULIMA wa kahawa Kaunti ya Embu, wanaomba Waziri wa Kilimo, Peter Munya aingilie kati ili asaidie kusuluhisha mgogoro wa muda mrefu kati ya wanachama wa chama cha ushirika cha kahawa cha Muruwe na usimamizi wao kuhusu mkopo wa Sh66 milioni.
Haya yanajiri baada ya mzozo kuzuka katika mkutano ulioandaliwa Ijumaa baina ya wanachama na wasimamizi wa chama hicho kusuluhisha mzozo huo na kufanya ufutiliwe mbali.
Kikao hicho kiliitishwa na Mkurugenzi wa Ustawi wa Vyama vya Ushirika ili kuwawezesha wakulima waliogawanyika kupiga kura kuamua iwapo watafanya uchunguzi kuhusu mkopo wa Sh66 milioni uliochukuliwa na usimamizi.
Wakulima hao wanadai kuwa wasimamizi walikosa kuwafahamisha kuhusu mkopo huo na hata kukosa kuonyeshwa rekodi ya jinsi walivyozitumia pesa hizo.
Hata hivyo, si wakulima wote waliokubaliana na pendekezo hilo lililotolewa Desemba 2021, huku baadhi yao wakitaka ukaguzi wa kitaalamu ufanyike jambo ambalo lilifanya mkurugenzi huyo kuitisha kikao cha wakulima kupiga kura ili kumaliza mzozo huo.
Wasimamizi wanashutumiwa kwa kuchukua mkopo huo bila kuidhinishwa na wanachama, huku wengi wao wakidai pesa hizo zilizitiwa mifukoni na watu binafsi na kuwaachia wakulima gharama ya kulipa mkopo huo.
“Tumepoteza imani kabisa na wasimamizi wetu na tunapinga pendekezo lao kuendelea kushikilia ofisi,” akasema Joseph Kanyi, mmoja wa wakulima hao.