• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 2:31 PM
Drama mzoga wa paka ukiondolewa dukani

Drama mzoga wa paka ukiondolewa dukani

NA MWANGI MUIRURI

KULIZUKA kizaazaa katika duka moja mjini Nyeri mnamo Alhamisi, Julai 27, 2023, baada ya majirani kuwaita maafisa wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) wakishuku mhudumu alikuwa ameaga dunia akiwa ndani.

Lakini maafisa hao walipofika wakiwa na vifaa vyote vya kufanya kazi yao na kuchukua sampuli, kisha wakavunja mlango wa duka hilo, walikumbana na mzoga wa paka mkubwa mweupe aliyekuwa akioza kwa kona moja ya duka hilo.

Gari la polisi lililofika kubeba mzoga wa paka mkubwa mjini Nyeri. PICHA | MWANGI MUIRURI

Wenyeji walisema kuwa duka hilo humilikiwa na mwanamke ambaye alikuwa hajaonekana kwa wiki nzima hivyo basi kuingiwa na wasiwasi wakati walianza kupigwa na mawimbi ya uvundo uliohanikiza kutoka kwa jengo hilo huku nzi wakitua kwa fujo.

“Tuliingiwa na wasiwasi na hata kisaikolojia tulianza kujiandaa kwa matanga. Tuliita maafisa wa polisi waje watusaidie kutwaa mwili. Ndipo maafisa wa DCI walifika na wakavunja mlango. Ndani ya duka hilo, ulipatikana mzoga wa paka mkubwa wa rangi nyeupe,” akasema Eustace Ngunjiri, mwenyeji wa eneo hilo.

Polisi walimfunika kwa shuka na wakambeba hadi kwa gari lao na wakampeleka kwa maabara kumtekelezea uchunguzi zaidi.

Ripoti ya maafisa hao katika kituo cha Central ilisema kwamba mtaalamu wa masuala ya mifugo atatekelea paka huyo upasuaji wa mzoga ili kubaini kilichomuua.

“Aidha, mwenye duka hilo tulimpigia simu na akatufahamisha kwamba alikuwa katika likizo mjini Mombasa na hakuwa na ufahamu wa paka ndani ya duka lake,” ikasema ripoti hiyo.

  • Tags

You can share this post!

Manchester United hoi Arsenal ikifinya Barca kirafiki

Aliyemuua mkewe kwa kumpakulia wali bila nyama afungwa...

T L