• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 5:50 AM
Vyakula vinavyoweza kukupa ngozi inayong’aa

Vyakula vinavyoweza kukupa ngozi inayong’aa

NA MARGARET MAINA

[email protected]

SIRI ya mja kuwa na ngozi inayong’aa iko kwa chakula.

Aghalabu sisi sote tunataka ngozi nzuri, laini na inayong’aa. Jinsi unavyolisha mwili wako ndivyo unavyolisha ngozi yako.

Ngozi ni kiungo kikubwa zaidi katika mwili kinachotupa dalili za mabadiliko ambayo yanaweza kutokea kwa mwili wetu wa ndani.

Chunusi, vipele, na ngozi kavu ni ishara kwamba mwili unakosa vitu fulani. Chakula unachokila hatimaye huakisi ngozi yako.

Unaweza kujumuisha vyakula tofauti ili uwe na ngozi inayong’aa.

Sharubati ya figili

Figili husaidia kusafisha damu na kuondoa taka za ngozi. Huongeza maji bora ambayo yanahitajika kwa ngozi nyororo.

Tango

Matango yana vitamini C, silika, potasiamu na magnesiamu. Silika, hasa katika ngozi ya tango, huboresha rangi na afya ya ngozi ya mwili. Tango pia huwa na maji mengi. Haya maji huingia kwenye ngozi kiasili na husaidia kuifanya iwe ni yenye kung’aa.

Mboga za majani na hasa za kijani

Mboga za majani mchicha na brokoli zimejaa virutubishi vya kusaidia ngozi ambavyo husaidia kuondoa sumu mwilini. Nyingi za mboga hizi zina vitamini A, B, C, E na K ambazo hukuza ngozi ya ujana na kuzuia mikunjo.

Vyakula vya rangi za chungwa, njano na nyekundu

Vyakula kama vile karoti, viazi vikuu na pilipili nyekundu au ya njano vina vitamini A na C zinavyong’arisha ngozi. Vyakula vya rangi ya machungwa, haswa, vina Beta carotene ambayo inajulikana kusaidia afya ya macho. Beta carotene inabadilishwa kuwa vitamini A ambayo inakuza ngozi ya ujana. Vitamini A husaidia kupunguza uharibifu wa ngozi kutokana na miale ya jua, ishara za kuzeeka na kuzuia mikunjo. Vyakula hivi pia vina vitamini C nyingi ambayo husaidia kutengeneza na kutengeneza upya kolajeni ya ngozi.

Tangawizi

Masuala mengi ambayo yanahusiana na ngozi yanaweza kuunganishwa na aina fulani ya kichochezi katika mwili. Kuvimba kwa ndani kunaweza pia kujidhihirisha kwenye ngozi kwa nje kama chunusi au upele wa ngozi. Tangawizi husaidia kupunguza uvimbe, huboresha ufanyaji kazi wa ini, na kusaidia kuweka ngozi yenye afya na laini.

Kabichi

Kabichi ina baadhi ya virutubisho vya kuondoa sumu kwenye ini. Kabichi inaweza kusaidia ngozi iliyokabiliwa na chunusi kwa sababu inasaidia kuondoa sumu mwilini mwako na kuziondoa kwenye mkondo wa damu. Kabeji pia ina vitamini A, C, na E. Virutubisho hivi bora vya kuzuia kuzeeka husaidia kulainisha ngozi na kupunguza mikunjo.

  • Tags

You can share this post!

Omanyala afanya mazoezi nchini Ufaransa kabla ya Rabat...

Man-United wazamisha Chelsea 4-1 katika EPL ugani Old...

T L