NA MASHIRIKA
WASHINGTON DC, AMERIKA
KUNDI la waasi la M23 limeonyesha hali ya kusitasita kuhusu ikiwa litashiriki kwenye juhudi za kurejesha amani katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na ukanda wa Afrika Mashariki, au la.
Hili ni licha ya viongozi kadhaa wa nchi shirika za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kusema kuwa waasi hao wako huru kushiriki katika mazungumzo hayo.
Hali hiyo iliibuka katika mkutano uliofanyika jijini Washington D.C., Amerika, ambako viongozi wa Afrika walikuwa wamehudhuria Kongamano la Amerika na Afrika.
Marais Evariste Ndayishimiye (Burundi), Paul Kagame (Rwanda), William Ruto (Kenya) na Samia Suluhu wa Tanzania walikuwa wamekutana katika mkutano mdogo baina ya viongozi wa eneo la Maziwa Makuu kujadili mizozo na mapigano yanayoendelea DRC.
Juhudi hizo za amani eneo la Maziwa Makuu zinaongozwa na rais wa Angola, Joao Lourenco, ijapokuwa zimeunganishwa na zile za EAC, inayoongozwa na Rais Ndayishimiye.
“Amani katika eneo hili ni jambo la dharura sana. Hatutakubali kupumzika hadi pale amani ya kudumu itarejea mashariki mwa DRC,” akasema Rais Ndayishimiye baada ya mkutano huo.
Akaongeza: “Tuliwasilisha mapendekezo yetu ya mwisho kwa Rais Felix Tshisekedi kwa hivyo tunatarajia M23 kuanza kuwapokonya silaha wanachama wake.
Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Kenya, Dkt Alfred Mutua, alisema eneo hili linataka mikataba iliyofikiwa nchini Angola na Kenya kutekelezwa, kama hatua ya kwanza ya kurejesha amani.
“Viongozi walikubaliana kuwa ni muhimu wadau wote katika mzozo huo kuzungumza pamoja ili kupata suluhisho la mzozo huo,” akasema Dkt Mutua.
Akaongeza, “Mkutano huo ulibuni mbinu nne ili kuharakisha mchakato wa kutafuta amani na kuwapa viongozi tofauti majukumu mbalimbali. Hili linajumuisha ufuatiliaji kuhusu utekelezaji wa mikataba hiyo ili juhudi hizi zipate mafanikio.”
Katika mkataba uliofikiwa jijini Luanda, nchini Angola, Rwanda na DRC ziliahidi kuanza mazungumzo ya pamoja.
Mataifa hayo yamekuwa yakilaumiana kuhusu ufadhili wa makundi tofauti ya waasi.
Mkataba uliotiwa saini jijini Nairobi, Kenya, uliyarai makundi yote yenye silaha kuanza mazungumzo na serikali ya DRC ili kupata amani.
Hata hivyo, M23 haikuhudhuria hafla ya kutiwa saini kwa mkataba huo.Pia, Dkt Mutua hakutoa ufafanuzi kuhusu mbinu hizo nne, ijapokuwa alisisitiza kuhusu umuhimu wa wadau wote kuzingatia masuala yaliyopitishwa kwenye makubaliano hayo.
Mapema Alhamisi, M23 ilisema mapigano mapya yalikuwa yameanza katika eneo la Bwiza, Kivu Kaskazini, huku ikililaumu jeshi la DRC dhidi ya “kushambulia ngome zake”.
Msemaji wa kisiasa wa M23, Laurence Kanyuka, alisema jeshi lenyewe ndilo “linahujumu juhudi za kurejesha amani”.
Jumanne wiki iliyopita, pande hizo mbili zilifanya kikao katika eneo la Kibumba, Kivu Kaskazini, ambapo zilikubaliana kudumisha amani.
Subscribe our newsletter to stay updated