Na MASHIRIKA
LILONGWE, Malawi
SERIKALI ya Malawi ilisema kuwa mabalozi wake kadhaa walitimuliwa kutoka Afrika Kusini baada ya kupatikana na hatia ya ulanguzi wa pombe ambayo haijatozwa ushuru.
Wizara ya Masuala ya Kigeni nchini Malawi eneo la Lilongwe ilisema Ijumaa kuwa taifa la Afrika Kusini limewapa mabalozi hao na familia zao saa 72 kuondoka nchini humo.Kupitia taarifa, Wizara ya Mahusiano ya Kimataifa Afrika Kusini ilisema kuwa uamuzi huo ulitekelezwa kwa sababu maafisa hao:
“Walipatikana na hatia ya kujihusisha na biashara haramu inayohusu pombe ambayo haijalipiwa ushuru,” kufuatia uchunguzi wa kina kuhusu madai ya kukiuka haki zao za kidiplomasia.Pretoria ilisema shughuli za kuchunguza madai sawa na hayo yanayohusu wajumbe wengine wa kigeni nchini humo “zinakaribia kukamilishwa na hatua sawa na hiyo itachukuliwa dhidi yao ikiwa watapatikana na hatia.”
Wizara ya Kigeni Malawi ilisema “imesikitika” kwamba mabalozi wa taifa hilo wametangazwa kama watu wasiotakikana” na ikaahidi kuchukua hatua za kinidhamu maafisa hao watakaporejea nyumbani.Mabalozi kadhaa wa Lesotho walifukuzwa kutoka Afrika Kusini Alhamisi kwa misingi sawa na hiyo.