NA MASHIRIKA
KINSHASHA, DRC CONGO
TAKRIBAN watu 141 walifariki na wengine kujeruhiwa kufuatia mafuriko na maporomoko ya ardhi yaliyosababishwa na mvua kubwa katika mji mkuu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Kinshasa.
Kutokana na mafuriko, barabara kuu ya N1 inayounganisha Kinshasa na bandari kuu ya bahari ya Matadi pia imeporomoka.
Kando na hayo, nyumba kadhaa pia zimesombwa na maji, jambo lililofanya wengi kupoteza makao.Ofisi ya Waziri Mkuu ilisema katika taarifa kwamba barabara hiyo inaweza kufungwa kwa muda wa siku nne.
“Shughuli za usafiri huenda zikaathirika zaidi kufuatia janga hili. Japo wengi wanategemea barabara hiyo, hatuna budi ila kuifunga kwa kipindi cha siku nne,” ikasoma taarifa kutoka kwa Waziri Mkuu.
Waziri wa Afya Jean-Jacques Mbungani Mbanda alisema kwamba wizara hiyo inaendelea kutathmini idadi kamili ya watu waliofariki.Alisema kuwa huenda idadi ya watu waliokufa ikaongezeka.
“Japo kwa sasa idadi ya waathiriwa ni zaidi ya 120, tunaendelea kuhesabu walioangamia kwenye janga hili,” akasema Mbanda.
Mafuriko ya mara kwa mara katika nchi hiyo yanahusishwa na maendeleo ya haraka na udhibiti duni.
Kwa upande mwingine, janga hilo linahusishwa na mabadiliko ya tabia nchi.Kulingana na maafisa watatu wa eneo hilo, takriban watu milioni 12 wanaishi katika vitongoji 24 vya Kinshasa vilivyoathiriwa na mafuriko.
Katika eneo la Ngaliema, zaidi ya watu 36 walifariki na miili bado inaendelea kuhesabiwa, kulingana na meya wa eneo hilo, Alid’or Tshibanda.
Picha zilizosambazwa kwenye mitandao ya kijamii zilionyesha maporomoko ya ardhi katika wilaya ya Mont-Ngafula yenye vilima.
“Hatujawahi kuona mafuriko hapa kwa kiwango hiki. Tumepoteza kila kitu,” akasema Blanchard Mvubu, mkazi wa Mont-Ngafula.
Waziri mkuu na gavana wa mkoa walizuru maeneo yaliyofurika, na maafisa wa eneo hilo wanatarajiwa kukutana na wawakilishi wa wizara ya mambo ya ndani na mashirika mengine ya serikali kushughulikia dharura hiyo.
Takriban watu 39 walifariki mjini Kinshasa mwaka wa 2019 wakati mvua kubwa ilinyesha katika maeneo ya mabonde na baadhi ya majengo na barabara kuporomoka.
Baada ya kupokea habari kuhusu vifo vya watu wake, Rais wa nchi hiyo, Félix Tshisekedi, alisema atakatiza safari yake nchini Amerika ili kuwafariji waathiriwa.
Katika ujumbe wake kwenye mtandao wa kijamii Tshisekedi alisema atarejea nyumbani leo baada ya kukutana na Rais Joe Biden.Rais huyo pia ametangaza siku tatu za maombolezo ya kitaifa.
Subscribe our newsletter to stay updated