• Nairobi
  • Last Updated May 13th, 2024 7:02 PM
Mhadhiri motoni kwa kushiriki ngono na mwanafunzi

Mhadhiri motoni kwa kushiriki ngono na mwanafunzi

Na AFP

RABAT, MOROCCO

MAHAKAMA moja nchini Morocco, Jumatano ilimhukumu mhadhiri wa chuo kikuu miaka miwili gerezani, kwa madai ya kushiriki ngono na mwanafunzi ili kumpa alama za juu kwenye mtihani wake.

Kulingana na vyombo vya habari nchini humo, ni mara ya kwanza kwa mtu kufungwa gerezani kuhusiana na shtaka kama hilo.

Kesi hiyo ilianza Septemba 2021 ambapo imekuwa ikifuatiliwa kwa ukaribu na vyombo vya habari.

Mshtakiwa ni mhadhiri wa Somo la Uchumi katika Chuo Kikuu cha Hassan I, Settat, karibu na jiji la Casablanca.

Kisa hicho kilifichuka Septemba, baada ya wanafunzi kuweka mitandaoni picha zilizoonyesha mazungumzo yaliyoaminika kuwa ya mhadhiri na mwanafunzi huyo.

Kulingana na uamuzi wa mahakama, mshtakiwa alipatikana na makosa ya “kumpiga mwathiriwa na kumdhulumu kimapenzi.”

Wahadhiri wanne zaidi wanatarajiwa kufikishwa mahakamani kwa mashtaka kama hayo.

Wanakabiliwa na mashtaka kuhusu “dhuluma za kimapenzi dhidi ya wanawake.”

Visa vya wahadhiri kushiriki ngono na wanafunzi vimekuwa vikiripotiwa kwa wingi katika siku za hivi karibuni nchini humo.

Mashirika ya kutetea haki za binadamu yanasema visa vya dhuluma za kimapenzi vimekuwa vikiongezeka sana katika nchi hiyo ingawa wanawake wengi hawajakuwa wakijitokeza kuripoti.

Mnamo 2018, Morocco ilibadilisha sheria zake kwa kuweka adhabu kali dhidi ya wale wanaopatikana kuwadhulumu kimapenzi wanawake.

You can share this post!

Chipukizi sita katika timu ya taifa ya wanaume

Wakazi wataka bomba la majitaka likarabatiwe upesi

T L