NA MASHIRIKA
LIMA, PERU
BUNGE la Peru limemuondoa madarakani Rais Pedro Castillo na nafasi yake kuchukuliwa na makamu, Dina Boluarte, muda mfupi baada ya kiongozi huyo kuidhinisha kuvunjwa kwa bunge la Congress.
Kulingana na ripoti ya polisi, rais huyo alikamatwa baada ya kuondolewa madarakani na kupelekwa katika kituo cha polisi cha Lima ambapo aliyekuwa rais Alberto Fujimori ambaye aliondolewa madarakani mnamo 2000 kwa sababu ya ufisadi amefungwa.
Baada ya kukamatwa kwake kutangazwa rasmi, polisi walianza kumchunguza kwa ‘uasi’.
Boluarte aliapishwa chini ya saa mbili baada ya kura ya kumuondoa madarakani Castillo kukamilika akiwa amevalia taji la urais mbele ya Bunge la Congress.
Akizungumza baada ya kuapishwa na wabunge, Boluarte alisema kuwa ataendelea kutumikia nchi hiyo bila ubaguzi.
“Kulikuwa na jaribio la mapinduzi ambalo halikupata uungwaji mkono wowote katika taasisi za kidemokrasia au mitaani,” akasema Boluarte.
Alisema anakusudia kutumikia muhula uliosalia wa Castillo, hadi Julai 2026. Hata hivyo, Ofisi ya mpatanishi mkuu wa kitaifa imelitaja jaribio la Castillo la kuvunja bunge kama mapinduzi.
Eduardo Gamarra ambaye ni mtaalamu wa masuala ya siasa na pia mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Florida alisema bunge la Peru lina uwezo wa kumuondoa rais madarakani.
Kadhalika, mtalaamu huyo alisema kuwa rais ana uwezo wa kulivunja bunge, kwa hivyo hatua ya Castillo haikuwa mapinduzi.
“Rais ana uwezo wa kulivunja bunge. Rais huyo hakufanya kosa,” akasema Castillo.
Wabunge 101 dhidi ya sita waliidhinisha kuondolewa kwa Castillo kutoka ofisini kwa madai ya utovu wa maadili.
Hata hivyo, wabunge 10 hawakushiriki katika kupiga kura.
Kwa upande mwingine, serikali ya Amerika ilikaribisha uteuzi wa Boluarte kama rais wa Peru, ambaye tayari ameapishwa na bunge la taifa.
Taarifa ya wizara ya mambo ya nje imepongeza udhabiti wa taasisi za Peru kwa kudumisha demokrasia na kusema kuwa itaendelea kuliunga mkono taifa hilo chini ya serikali ya umoja wa kitaifa.
Si mara ya kwanza nchi hiyo kukosa utulivu wa kisiasa.
Tangu mwaka wa 2016, nchi hiyo imekuwa na marais 6.
Castillo alichaguliwa kuwa rais 2021 baada ya kumshinda Keiko Fujimori, bintiye rais wa zamani aliyefungwa baada ya kupatikana na hatiya ya ufisadi.
Subscribe our newsletter to stay updated