NA AFP
LAGOS, NIGERIA
UHESABU wa kura uliendelea jana Jumapili nchini Nigeria, siku moja baada ya raia nchini humo kushiriki kwenye uchaguzi mkuu wa kihistoria wenye ushindani mkali.Ushindani mkuu unatarajiwa kuwepo baina ya wawaniaji watatu wakuu wa urais.
Jumla ya wapigakura 90 milioni walishiriki kwenye uchaguzi huo, ambao ulifanyika kwa njia ya amani, ijapokuwa kulikuwa na baadhi ya visa vichache vya ghasia, ucheleweshaji wa vifaa na matatizo ya kimitambo.
Kutokana na matatizo hayo, watu wengi walilazimika kungoja hadi nyakati za usiku ili kupiga kura.Baada ya mihula miwili ya Rais Muhammadu Buhari, raia wengi wameeleza matumaini yao kuwa kiongozi mpya watakayemchagua atachukua hatua madhubuti katika kukabili ukosefu wa usalama, ukosefu wa ajira na ongezeko la umaskini.
Uchaguzi huo unaonekana kuwa ushindani baina ya meya wa zamani wa Lagos, Bola Tinubu, anayewania kwa tiketi ya chama cha APC, dhidi ya makamu wa rais wa zamani, Atiku Abubakar, anayewania kwa tiketi ya chama cha PDP.
Tinubu ana umri wa miaka 70 huku Atiku akiwa na umri wa miaka 76.Hata hivyo, kwa mara ya kwanza tangu kukamilika kwa utawala wa kijeshi mnamo 1999, mwaniaji wa tatu, Peter Obi wa chama cha Labour, anaonekana kuzua ushindani dhidi ya vyama vya APC na PDP kwa kutoa ahadi ya kuleta mabadiliko nchini humo ikiwa atachaguliwa kuwa rais.
Umati wa watu ulipiga kambi katika vituo tofauti vya kupigia kura jijini Lagos na miji mingine mikuu Jumamosi, huku maafisa wa uchaguzi wakianza rasmi uhesabu wa kura. Baada ya matokeo kunakiliwa katika vituo hivyo, yanatumwa katika kituo kikuu.
“Tumemaliza kuhesabu, japo lazima tuhakikishe kuwa wameyaweka matokeo kwenye tovuti ya tume ya uchaguzi,” akasema Chizoba Onuoha, ambaye ni msimamizi wa masuala ya mitambo (ICT) katika kituo kimoja jijini Lagos.
Kutokana na ushindani mkubwa uliopo, baadhi ya wachanganuzi wanatabiri kwamba huenda kukawa na duru ya pili ya uchaguzi kati ya washindani wakuu wawili, ikiwa hakutakuwa na mgombea atakayefikisha idadi ya kura inayohitajika.
Kwa baadhi ya wapigakura, iliwalazimu kungoja zaidi hata nyakati za usiku kwani mitambo ya kuwatambua ilikosa kufanya katika baadhi ya vituo jijini Lagos na sehemu nyinginezo.
Katika jiji la Kano, lililo kaskazini magharibi mwa taifa hilo, vifaa vya kupigia kura viliwasili saa tano baada ya vituo kufunguliwa.
“Upigaji kura bado unaendelea hata baada ya muda rasmi wa kupiga kura kukamilika,” akasema Kabiru Sani, 37, ambaye ni miongoni mwa wapigakura walioshiriki kwenye uchaguzi huo.
“Tulianza tukiwa tumechelewa. Hivyo, hatutakubali uamuzi wowote wa kutuzuia kupiga kura hata baada ya muda uliowekwa kukamilika.”
Subscribe our newsletter to stay updated