NA AFP
LAGOS, NIGERIA
NIGERIA imetangaza matokeo ya mwanzo baada ya uchaguzi wenye ushindani mkali katika taifa lenye idadi kubwa ya watu zaidi Afrika.
Uchaguzi huo ulikumbwa na ucheleweshaji na madai ya majaribio ya wizi wa kura.
Karibu watu 90 milioni walishiriki kwenye uchaguzi huo Jumamosi kumchagua kiongozi atakayemrithi Rais Muhammadu Buhari.
Wengi wameeleza matarajio yao kuwa kiongozi wao mpya atakabiliana na ukosefu wa usalama, changamoto za kiuchumi na hali ya juu ya umaskini.
Uchaguzi huo uliendelea vizuri na kwa amani katika sehemu nyingi, licha ya matatizo machache kushuhudiwa katika baadhi ya vituo vya kupigia kura.
Uchaguzi huo unaonekana kuwa wenye ushindani mkuu baina ya meya wa zamani wa Lagos, Bola Tinubu, 70, wa chama tawala cha All Progressives Congress (APC) dhidi ya aliyekuwa makamu wa rais wa taifa hilo Atiku Abubakar, 76, wa chama cha Peoples Democratic Party (PDP).
Lakini kwa mara ya kwanza tangu kukamilika kwa utawala wa kijeshi mnamo 1999, mwaniaji wa tatu, Peter Obi wa chama cha Labour pia anaonekana kuzua ushindani mkali dhidi ya wawaniaji hao wawili.
Obi amekuwa akiendeleza jumbe za kuwavutia vijana.
Ikitoa tangazo la kwanza jimbo hadi jimbo, Tume Huru ya Kitaifa ya Uchaguzi (INEC) hapo jana Jumatatu, Tinubu wa APC alipata ushindi katika jimbo dogo la Ekiti huku chama cha PDP kikiibuka cha pili.
Hata hivyo, matokeo hayo ni ya mwanzo tu katika taifa hilo lenye mgawanyiko mkubwa baina ya Waislamu katika eneo la kaskazini na Wakristo katika eneo la kusini.
Matokeo ya uchaguzi nchini humo huwa yanaamuliwa na majimbo makubwa kama vile Lagos, Kanu na Kaduna.
Ili kutangazwa mshindi wa urais, lazima mwaniaji urais apate angaa asilimia 25 ya kura zilizopigwa katika thuluthi mbili ya majimbo 36 ya taifa hilo.
Hata hivyo, hatua ya tume hiyo kuchelewa kuweka matokeo hayo kwenye tovuti yake jana kulizua hofu ya wizi wa kura kutokea.
Madai hayo yamekuwa yakitolewa kwenye chaguzi kadhaa ambazo zimefanyika nchini humo hapo awali.
“Acha raia wa Nigeria waamue! Usijaribu kugeuza matokeo yoyote,” akasema mwanamuziki maarufu Burna Boy.
Mwaniaji wa chama cha PDP, Abubakar, aliirai tume hiyo kuweka matokeo kwenye tovuti yake mara moja baada ya kuyapokea. Aliwalaumu baadhi ya magavana wa majimbo kwa kujaribu kubadilisha matokeo hayo.
“Itakuwa vibaya ikiwa yeyote atajaribu kubadilisha maamuzi ya raia kwa kubadilisha matokeo ya uchaguzi,” akasema kwenye taarifa.
Aliposhindwa kwenye uchaguzi mkuu wa 2019, Abubakar alidai kuwa uwepo wa udanganyifu, lakini kesi yake ilifutiliwa mbali na Mahakama ya Upeo.
Mwenyekiti wa chama cha Leba, Julius Abure, pia aliwalaumu baadhi ya maafisa wa uchaguzi kwa kukosa kuweka matokeo hayo kimakusudi katika tovuti.
Subscribe our newsletter to stay updated