NA MASHIRIKA
COVID-19 si tena janga la dharura kimataifa, Shirika la Afya Duniani (WHO) limetangaza Ijumaa, Mei 05, 2023 kuashiria hatua kubwa iliyopigwa tangu ugonjwa huo kugunduliwa Wuhan, China mnamo Desemba 2019.
Mkurugenzi Mkuu wa WHO Tedros Adhanom Ghebreyesus ametangaza kwamba shirika hilo kama tu mataifa kote ulimwenguni limejifunza mengi kuhusu namna ya kukabiliana na majanga ya afya.
“Jana (Alhamisi) Kamati ya Dharura ya Janga la Covid-19 ilikutana kwa mara yake ya 15 na ikanipendekezea kwamba nitangazia umma wote wa ulimwengu kwamba Covid-19 si tena janga la dharura kimataifa. Nimekubali ushauri huo. Kwa matumaini makubwa ninatangaza kwamba Covid-19 si tena suala la dharura kote ulimwenguni,” amesema Ghebreyesus.