• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 1:01 PM
Viongozi wamuomboleza mume wa Malkia Elizabeth

Viongozi wamuomboleza mume wa Malkia Elizabeth

Na AFP

LONDON, Uingereza

VIONGOZI mbalimbali duniani wanaendelea kuomboleza kifo cha mumewe Malkia wa Uingereza Elizabeth II, Mwanamflame Philip, ambaye ni kiongozi wa ufalme wa Uingereza.

Marehemu mwanamflame Philip aliaga dunia mnamo Ijumaa akiwa na miaka 99 baada ya kuugua kwa muda mrefu.

Aliyekuwa Rais wa Marekani, Barack Obama alikuwa kati ya viongozi wa kwanza waliomwomboleza Philip, akimtaja kama mtu mpole ambaye alitangamana na viongozi wote kwa usawa bila kujali hadhi kubwa aliyokuwa nayo katika jamii.

Mnamo 2011, Rais Obama aliishi katika Kasri la Buckingham kwa siku mbili na kushiriki chajio na familia hiyo ya ufalme. Aidha alikumbuka jinsi alivyokutana na Philip na mazungumzo yao katika ikulu hiyo wakati wa kongamano la mataifa yenye uchumi mkubwa, G20 mnamo Aprili 2009.

“Alikuwa mkarimu kama walivyokuwa wanasiasa wenye sifa kubwa kihistoria kama Winston Churchil, Kennedy, Nelson Mandela na Gorbachev. Ziara yetu katika Kasri la Buckingham ilikuwa ya heri kwa kuwa Philip alitangamana na wote vizuri licha ya kuwa kati ya watu wenye ushawishi na heshima kuu duniani,” akasema Rais Obama.

Marais wa Afrika hawakuachwa nyuma, wengi wakituma rambirambi zao kwa malkia Elizabeth 11 na kumsifia Philip.

“Zambia inaungana na nchi nyingine kutuma rambirambi kwa familia ya Ufalme wa Uingereza kufuatia kifo cha Philip. Alikuwa mtu mwenye utu na kiongozi mwenye hekima ambaye aliishi miaka mingi na kuwasaidia watu wengi duniani,” akasema Rais wa Zambia Edgar Lungu.

Rais wa Nigeria Muhammadu Buhari pia alimwomboleza Philip akimtaja kama kiongozi wa ulimwengu ambaye aliishi maisha tulivu ndani ya ufalme na alikuwa mkarimu aliyewasaidia watu wasiojiweza.

“Alihusika katika kufadhili miradi ya vijana na kutunza wanyamapori. Ukarimu wake umehakikisha kuwa nchi za Afrika zinapata ufadhili wa miradi mbalimbali kutoka Uingereza,” akasema Rais Buhari.

Ufalme wa Eswatini pia ulituma rambirambi zao kupitia wizara ya kigeni, wakisema maisha ya Philip katika ufalme wa Uingereza ulifungua milango ya misaada kwa nchi nyingi za kiafrika.

“Alisifiwa na vizazi vyote Marekani, mataifa ya Jumuiya ya Madola na Duniani. Hasa ukarimu wake utakumbukwa daima dawamu,” ikasema taarifa kutoka Ufalme wa Eswatini.

Aliyekuwa Rais wa Liberia Ellen Johnson Sirleaf na mwenzake wa Botswana Ian Khama walimiminia sifa marehemu, wakisema kifo chake ni pigo kuu kwa mataifa yaliyoko chini ya Jumuiya ya Madola.

You can share this post!

Walibora akumbukwa kwa kongamano

FUNGUKA: ‘Usinihukumu; napenda kuvalia mavazi ya kike’