• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 10:08 PM
AKILIMALI: Mkulima anavyochuma kutokana na matundadamu

AKILIMALI: Mkulima anavyochuma kutokana na matundadamu

Na PETER CHANGTOEK

MATUNDADAMU yenye rangi nyekundu yananing’inia kwa mimea katika shamba moja lililoko katika eneo la Ainabkoi, katika Kaunti ya Uasin Gishu.

Mja anapoingia katika shamba hilo, huvutiwa na matunda hayo yanayomfanya yeyote kutokwa na mate mdomoni, anapoyatazama.

Elisha Onzilu, 40, ni mwenye mimea hiyo iliyonawiri. Isitoshe, ana shamba jingine katika eneo la Nyaru – takriban kilomita 47 kutoka mjini Eldoret – katika Kaunti ya Elgeyo Marakwet, na jingine eneo la Kipkabus, Kaunti ya Uasin Gishu.

Kwa jumla, Onzilu ana mimea ya matundadamu katika ekari tano anakochuma kati ya kilo 700 hadi 1,000 za matunda hayo kila baada ya wiki mbili kwa kila ekari.

Onzilu alipokuwa shuleni walikuza matundadamu shambani mwao, ila yalikuwa machache tu ya kuliwa.

Pindi alipokamilisha kidato cha nne mnamo 2,000 alijipa shughuli ya kukuza miche ya mivinje, mikalatusi na mingineyo kabla kujitosa katika matundadamu

Aliuza miche hiyo kwa taasisi kadha za serikali. Hata hivyo, kiangazi kilipozidi 2010, soko la miche likanyauka akalazimika kugeukia aina nyingine ya kilimo ambayo ingempa fedha.

“Nikafanya utafiti kuhusu matundadamu, ambapo pia nilielekea Nairobi kuchambua soko,” asema na kueleza kuwa alianza na suala la soko kabla kuzamia shughuli hasa ya ukuzaji mimea hiyo.

Mnamo 2011, akawa anayanunua matundadamu kutoka kwa wakulima walioishi karibu naye na kuyauza.

“Nayanunua na kutumia wateja Nairobi. Nilipoona soko limepanuka niliomba wazazi nusu ekari ili nianze kukuza matunda yangu mwenyewe,” alihoji mkulima huyo.

Kilimo hicho alikichangamkia 2012, na muda si muda akaanza kuhesabu faida.

“Yalipoiva 2013 nikapata kampuni ya Fresh & Juice mjini Limuru, iliyokuwa imepewa tenda ya kuuzia duka la jumla la Nakumatt matundadamu.

“Mara moja nikaanza kuweka akiba na ilipofika 2016 nikanunua shamba la ekari moja kule Kipkabus kwa pesa hizo,” afichua na kusema alitumia mtaji wa Sh100,000 kuanzisha kilimo hicho.

Mbali na ya kwake Onzilu pia aliendelea kuyanunua ya wakulima wengine ili kuwaridhisha wateja wake, ambao sasa walikuwa wengi.

Ni hali iliyomfanya kuelekea Nairobi kutafuta nafasi ya kuwasilisha matundadamu kama mmoja wa saplaya wakubwa katika soko maarufu la matunda la Marikiti, na akafanikiwa.

Licha ya maduka ya Nakumatt kufungwa, hilo halikumwathiri kwani alikuwa ameshaanza kukita katika soko la Marikiti na pia lile la City Park, lililoko eneo la kifahari la Parklands mjini Nairobi.

Katika shamba lake la Kipkabus, mkulima huyu alichagua pia kukuza mikarakara. Hata hivyo, alipitia changamoto si haba.

“Mimea ilifagiliwa na magonjwa, faida ikaharibiwa na mfumkobei na kwa jumla ilinitoa jasho sana. Nikachuma tu miaka miwili 2017 na 2018,” aeleza baba huyu wa mtoto mmoja.

Mwaka 2018 alikodi shamba lingine la ekari mbili katika eneo hilo la Kipkabus, akalitumia kupanua kilimo chake cha matundadamu na sasa anaendelea kuyachuma.

“Kwa jumla, nina ekari tano za matundadamu; tatu katika Kaunti ya Uasin Gishu na mbili katika Kaunti ya Elgeyo Marakwet,” asema.

Aina ya Giant Red Oratia ndiyo huzaa matunda mengi; mmea mmoja hutoa kilo mbili kila baada ya wiki mbili. Mkulima anaweza kuchuma kilo 2,000 kwa shamba la ekari moja la aina hiyo.

Onzilu hupanda miche 1,200 katika ekari moja.

“Wakati wa upanzi tunatumia mbolea debe moja. Unaacha nafasi ya mita mbili kati ya mimea,” adokeza mkulima huyo.

Huchimba mashimo ya kina cha futi mbili na upana wa futi mbili, akachanganya mbolea asilia debe moja au mbili na mchanga uliotoka kwa mashimo hayo, akanyuyiza maji na kupanda miche.

Kila baada ya wiki mbili Onzilu huchuma matundadamu kati ya kilo 750 na 1,000 kutoka kwa ekari moja.

Mmea unapozaa matunda kwa mara ya kwanza, aghalabu, mavuno si mengi, lakini kadiri muda unavyozidi kusonga mbele ndivyo kiwango cha mazao kinazidi kuongezeka.

Mkulima huyo, ambaye pia huikuza miche ya matundadamu na kuwauzia wakulima wenzake, anasema janga la Covid-19 limeathiri soko la matunda hayo.

Hapo awali, alikuwa na mteja ambaye alikuwa akimchukua tani nzima ya matundadamu; lakini kwa sasa hununua kati ya kilo 300 na 400 pekee.

Aidha, kwa sasa anayauza matundadamu kwa bei ya kati ya Sh70 na 80 kwa kilo moja. Hapo awali aliyauza Sh100 kwa kilo.

Anasema uaminifu baina ya mwuzaji na mteja ni muhimu sana katika biashara.

“Nina wateja zaidi ya 20 katika soko la Marikiti lakini hatujawahi kuonana. Mimi huwatumia tu matunda nao hunitumia pesa,” aeleza.

Ilivyo kawaida, yeye hunyunyiza dawa kuua wadudu wanaovamia mimea hiyo.

Aidha, magonjwa kama vile Tree Tomato Mosaic ni hatari kwa matunda hayo.

Yote tisa, Onzilu asisitiza kilimo cha matundadamu kina faida zaidi ikilinganishwa na mimea mingine. Anapania kuongeza thamani kwa matunda yake katika siku zijazo.

You can share this post!

KINYUA BIN KING’ORI: Wapigakura wa kulaumiwa kuchagua...

AKILIMALI: Miaka 20 akizalisha ndizi, zina mapato ila Covid...