NA MARGARET MAINA
VIAZI mviringo au viazi ulaya ni baadhi tu ya majina yanayotumika kutofautisha zao hili na zao la viazi vitamu.
Viazi mviringo vinamfanya mtu kuhisi ameshiba
Kiazi kidogo kinaweza kuupatia mwili nguvu za kutosha kuliko vyakula vingine kama vile vitokanavyo na nafaka, samaki, nyama matunda na mbogamboga.
Viazi mviringo vina kiwango kikubwa cha madini ya potasiamu
Kiazi kidogo cha mviringo kinaweza kikawa na gramu nyingi za madini ya potasiamu. Hiki ni kiwango kizuri ambacho iwapo kitatumika kitasaidia katika mzunguko wa damu na kupunguza uwezekano wa kupata matatizo ya mzunguko wa damu kama vile presha na magonjwa ya moyo.
Viazi mviringo vina vitamini C kwa wingi
Kiazi mviringo chenye saizi ya kawaida kina uwezo wa kukupatia kiwango cha vitamini C unayohitaji kwa siku. Vitamini C ni muhimu katika mwili wa binadamu kwani husaidia katika kupambana na maradhi na kuimarisha ngozi na kuzuia kutoka damu kwenye fizi.
Viazi mviringo vina madini ya chuma
Ingawa viazi mviringo havitumiwi kama chanzo kikuu cha madini ya chuma, kiazi mviringo chenye saizi ya kawaida kinaweza kuupatia mwili asilimia kiasi fulani ya madini ya chuma yanayotakiwa kwa siku. Hii ni habari nzuri kwa wasiokula nyama. Madini ya chuma ni muhimu kwenye mwili wa binadamu kwani husaidia katika utengenezaji wa seli nyekundu za damu na usafirishaji wa hewa ya oksijeni mwilini.