• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 10:08 PM
FAUSTINE NGILA: Mitandao yabadili sura ya maandamano nchini

FAUSTINE NGILA: Mitandao yabadili sura ya maandamano nchini

NA FAUSTINE NGILA

KWA wiki nzima, Wakenya wamepiga kambi katika mitandao ya kijamii ya Twitter na Facebook kuishinikiza Hazina ya Kimataifa ya Fedha (IMF) kukoma kuikopesha Kenya pesa.

Wakenya walifoka kila aina ya matamshi kuonyesha kero lao kwa mtindo wa serikali wa kukopa mabilioni kila mwaka, wakidai hela hizo huibwa na maafisa wa serikali na kuwaacha kwa umaskini zaidi.

Hii ni aina mpya katika uanaharakati, ambapo wananchi wanatumia uwezo mkubwa wa teknolojia kutoa malalamishi yao na kuwafikia walengwa kwa muda mfupi.

Ni unaharakati ambao uliilazimisha IMF kuchapisha taarifa ndefu katika tovuti yake ikiwaelezea Wakenya sababu ya kuikopesha serikali ya Rais Uhuru Kenyatta Sh257 bilioni.

Kando na unaharakati wa zamani ambao hutegemea maandamano barabarani watu wakiinua mabango yenye maandishi ya kupinga sera, uanaharakati wa mitandaoni unaonekana kubadilisha kabisa matumizi ya nguvu na makabiliano na polisi barabarani.

Ni mtindo mpya ambapo wanaotetea haki zao hujificha chini ya majina feki kwenye Twitter na Facebook, hali inayowapa nguvu za kuandika kila aina ya maneno mazito na mabango ya kidijitali yenye jumbe kali.

Maandamano ya zamani yaliwatia hofu wanaharakati, hasa wale wenye biashara. Waliogopa kukomolewa na polisi, kushtakiwa baadaye au kupoteza wateja, kwa kuwa nyuso zao zingeonekana kwa runinga.

Ingawa IMF haikufuta uamuzi wake wa kuipatia Kenya mkopo, ilitambua shinikizo za kipekee ilipojaribu kuongoza mkutano wa mitandaoni Facebook ambapo Wakenya walifurika kuikumbusha Kenya ni taifa fisadi lisilojua kutumia vizuri hela za deni.

Kwenye tovuti mbadala, Wakenya walifikisha saini zaidi ya 200,000 kwenye jukwaa la ##SignThePetition wakitia presha IMF kusitisha mkopo ule.

Kwa kawaida, maandamano huongozwa na wanaharakati kama hamsini hivi lakini wiki iliyopita, kila Mkenya anayemiliki simu ya kisasa alichangia katika sauti ya pamoja ya kutangazia dunia kuwa Kenya inaongozwa na viongozi fisadi.

Kati ya Wakenya hao wote, ni mmoja tu, Mutemi Kiama, aliyekamatwa na polisi, ila yeye naye alichapisha bango la kidijitali la kijasiri zaidi ambalo serikali ilihisi lilikiuka sheria za maadili ya mitandaoni.

Ni picha ambayo ilichochea hisia miongoni mwa Wakenya, na kusambazwa katika kila kundi la WhatsApp, lakini hilo halikuzuia IMF kukatiza mchakato wa kuipa serikali mabilioni.

Kelele hizo zote ziligeuka kuwa za chura tu, zisizoweza kumzuia ng’ombe kunywa maji kwani Wakenya wengi hawakuchunguza kwa nini IMF ilikubali kutoa hela hizo.

Ni kweli kuwa asilimia kubwa ya pesa za mikopo huishia mifukoni ya maafisa wa ngazi za juu serikalini, lakini ingawa mitandao ya kijamii inawapa wananchi jukwaa la kukosoa serikali, wanafaa pia kufanya utafiti wa kina kuhusu sababu za maandamano yao.

Serikali ya Kenya haina uwezo wa kutoa hela kwa wananchi kukabili makali ya corona kama yalivyofanya mataifa yaliyoendelea, hivyo mkopo huo utatumika kuhakikisha hela zinasambaa katika uchumi, usije ukakosa huduma au bidhaa muhimu.

Hata hivyo, ni wito kwa maafisa wa serikali kukomesha wizi wa mabilioni ya pesa za wananchi. Lakini nao wananchi wasikome hapo, waanzishe hashtegi za kutimua wezi hao.

You can share this post!

JAMVI: Miungano ya kisiasa inayobuniwa nchini ni ya kufaidi...

KINYUA BIN KING’ORI: Rais Suluhu ametoa ishara...