• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 5:50 AM
HUKU USWAHILINI: Kwetu kuna wajuba magwiji wa kuwageuza akina dada walezi wao

HUKU USWAHILINI: Kwetu kuna wajuba magwiji wa kuwageuza akina dada walezi wao

NA SIZARINA HAMISI

HUKU tunakoishi kuna katabia kameshamiri hasa kwa baadhi ya wanaume.

Kwamba baadhi ya watu huanzisha uhusiano kwa lengo maalum la kupata mtu wa kutatua shida zao na wala sio mapenzi wala kupenda.

Tunawajua na tunawaona wanaume wa huku kwetu jinsi wanavyowinda akina dada ambao wanaonekana angalau hali zao za kimaisha zina ahueni na wengine hawafichi.

Wanasema wazi kwamba huko kuna heri na wanafanya kila wawezalo kuwanasa hao akina dada.Ndiposa tumezoea kuwaona wakijidai wana mapenzi ya dhati na wasichana wenye kazi ama shughuli zao mjini na ambao wanaishi maisha yenye afadhali huku Uswahilini.

Wanaume hawa wana mbinu za kivita, tena za nchi kavu na hata mwituni, kwani pale wanapopata msichana utawaona wakijidai wana mapenzi ya dhati, si ajabu kuwapata wanabeba hadi kibeti cha msichana katika harakati za kuonyesha kwamba wamependa hadi kituo cha mwisho.

Nao wasichana wasioelewa hawa wanaume huweza kudhani wamepata, kumbe wamepatikana. Huwa tunawaona jinsi wanavyowekeza mapenzi yao yote wakiamini wamepata mwenza wa maisha. Lakini kumbe huyo mwanamume ana malengo yake, hana mapenzi yoyote bali anajidai anapenda ili achune hadi aache msichana akiwa mtupu, mweupe kabisa, bila chochote.

Iwapo dada unahamia huku Uswahilini, uone kijana barobaro anakufuata nyuma kama nzi anavyofuata yasiyotamkika, tafakari mara mbili.

Hasa iwapo wewe ni msichana mwenye kazi yako inayokuingizia kipato na kila kukicha unafuatwa na wanaume ambao wanajidai wanakupenda na wanataka kuwa nawe, basi tia shaka. Usidhani kwamba umependwa sana na ukajihisi una bahati ya kuandamwa na wachumba watarajiwa.

Wajuba wa Uswahilini ni wabaya na tena hawana huruma, wanaweza kujeruhi moyo wako na ukaona dunia imekuinamia.

Hivyo dada mrembo ukiwa huku maeneo yetu, jitathmini tena mara mbili iwapo unajikuta umependa kiasi cha kushindwa kuona wala kusikia, kwani huenda umeingia kwenye penzi la kisanii la kutaka kugeuzwa mlezi. Hako kamchezo ka wanaume wengi kupenda kupata wanawake wa kuwalea kameshamiri sana.

Wapo wasichana walioerevuka na kuamka kabla ya kujikuta wametendwa, kwani tunawaona wengine wakiwa makini zaidi na hata wanapoingia katika uhusiano wanachunguza na wanachanganua.

Tunawasikia hawa wanaume wakijisifu vijiweni, jinsi msichana fulani alivyozimika kiasi kwamba anapewa chochote anachotaka. Na tena wanajigamba kwamba wakishahakikisha wamechuma vya kutosha, wanawatupa kama kaa la moto. Kuweni makini akina dada, mnachoona inaweza kuwa kiini macho.

[email protected]

  • Tags

You can share this post!

Wakufunzi wa KPL, KWPL roho juu Ligi zikirejea wiki hii

SHANGAZI SIZARINA: Mbona kila ninayemtongoza anikataa?

T L