• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 6:50 AM
JIJUE DADA: Kinachosababisha maumivu ya tumbo wakati wa hedhi

JIJUE DADA: Kinachosababisha maumivu ya tumbo wakati wa hedhi

NA PAULINE ONGAJI

MAUMIVU ya tumbo wakati wa hedhi husababishwa na kutanuka na kunywea kwa njia ya uzazi ili kuondoa damu kwenye kuta zake.

Hali hii husababishwa na homoni zinazochochea seli kwenye ukuta huu kuongezeka na kuwa nzito ili kujitayarisha kwa mimba.

Iwapo mwanamke hatashika mimba, basi sharti chembechembe (hedhi) hizi ziondolewe mwilini).

Aidha, kuna sababu zingine ambazo husababisha tumbo kusokota wakati wa hedhi, kama vile: Gesi au maji mengi katika sehemu ya chini ya tumbo wakati huu.

Tumbo kuvimba kutokana na matatizo ya mmeng’enyo wa aina fulani za vyakula.

Ingawa shida hii huwakumba baadhi ya wanawake kwa siku chache tu kila mwezi, wengi hushindwa kabisa kuendelea na shughuli za kawaida wakati huu. Mbinu hizi zitakusaidia kukabiliana na uchungu huu:

  • Maji moto: Tumia kitambaa kilichotumbukizwa kwenye maji moto kuchoma sehemu za chini za tumbo na mgongoni. Hii husaidia kutuliza misuli ya tumbo na hivyo kupunguza uchungu. Aidha, kuoga kwa maji moto yaliyochanganywa na mafuta iliyo na manukato pia itasaidia kukabiliana na shida hii.
  • Mazoezi: Mbali na kutuliza ubongo wakati wa hedhi, mazoezi ni muhimu kwa sababu hutanua misuli na hivyo kuimarisha mwenendo wa damu. Mazoezi kama yoga husaidia nyakati hizi kwani mbali na kutanua misuli, huiwezesha kutulia na hivyo kupunguza maumivu.
  • Chai moto: Chai moto huwa muhimu wakati huu kutokana na uwezo wake wa kutibu maumivu yanayotokana na kusokotwa na tumbo.
  • Lishe: Wakati wa hedhi, kuepuka na aina fulani ya vyakula kunaweza punguza maumivu ya tumbo. Vyakula vilivyo na viwango vya juu vya madini ya sodium na magadi vinapaswa kuepukwa kwani huchangia kuvimba na hivyo kuongeza maumivu ya tumbo. Ni muhimu kula vyakula vilivyo na viwango vya juu vya madini ya chuma. Pia, ni muhimu kuepuka vyakula ambavyo umegundua hukuongezea matatizo haya
  • Dawa: Kutumia dawa wakati wa hedhi husaidia kutuliza uchungu huu. Vilevile, kutumia dawa hizi unapokaribia siku za hedhi, kutakuepusha na uchungu huu. Lakini ni vyema kutafuta ushauri wa daktari kabla ya kuchukua hatua yoyote.
  • Onyo: Wakati mwingine maumivu haya wakati huu huzidi sana na yanaweza kujitokeza kama ishara ya shida kubwa, kwa mfano endometriosis (hali inayotokana na kuota kwa chembechembe za ukuta wa njia ya yai, katika sehemu zingine, mbali na njia ya uzazi). Ikiwa uchungu huu unakuzuia kuendelea na shughuli zako za kawaida, muone daktari kwa uchunguzi zaidi.
  • Tags

You can share this post!

MUME KIGONGO: Wanaume wanene hatarini kuathiriwa na maradhi...

Jinsi alivyoanzisha kituo cha michezo kuzuia watoto kuwa...

T L