NA SINDA MATIKO
PENZI la mwigizaji Frida Kajala na supastaa wa Bongo Flava Harmonize, linazidi kushika kasi ya 5G.
Kajala sio tu mpenzi wake lakini pia ndio meneja wa Konde Boy.
Wawili hao wamekuwa wakiposti video kadhaa wakifanya mazoezi ya pamoja, wakiwa studioni msela akirekodi ngoma na hata wakiwa viwanjani wakishuti mzigo.
Posti hizi zimeendelea kuibua hisia kali wengi wakionekana kumponda Kajala kwa kukubali kurudiana na jamaa ambaye aliwahi pia jaribu kutongoza binti yake Paula.
Lakini kama wanategemea atamwacha, mrembo huyo mwenye umri wa miaka 40 anasema kwa Harmonize ndiko habanduki hata wabaya wao wafanye nini.
“Kila siku nazidi kumpenda hata zaidi kwa sababu dunia nzima inapingana na sisi. Nampenda sana,” Kajala katamka.
Tayari ameshavishwa pete ya uchumba na anasema yupo tayari kufunga harusi na mzee baba.