NA SINDA MATIKO
JUZI Cristiano Ronaldo katangaza anauza ndege yake ya kibinafsi kwa sababu imekuwa ndogo kutokana na familia yake kupanuka. Sasa anataka kununua kubwa kidogo.
Ndio maisha waishiyo mastaa wengi. Huwezi ukawalaumu. Wengine baada ya kupiga pesa waliamua kustaafu kabisa. Hivi ukiwa na pesa zinazotosha kununua Kisiwa chako binafsi na yoti, na pipa, utasita kustaafu?
Kuna ambao walishaamua sanaa imetosha, wakajitoa ila kwa sababu moja au nyingine, iwe fedha au mapenzi ya sanaa, wakaamua kuoga na kurudi soko. Hawa Kwa mfano.
CAMEROON DIAZ
Astaafu: 2014
Arejea: 2022
Miaka minane baada ya kustaafu uigizaji, staa Diaz kaamua kurudi kwenye gemu mwaka huu. Filamu yake ya mwisho ilikuwa Annie aliyoigiza na Jamie Foxx ila sasa anarudi na mzigo mwingine Back In Action, utakaomshirikisha Foxx tena. Filamu hiyo itaanza kutengenezwa mwishoni mwa mwaka huu.
JULIA ROBERTS
Astaafu: 2002
Arejea: 2022
Huwezi kuamini Julia Roberts kaamua kurudi kwenye gemu baada ya miaka 20. Julia alistaafu hata kabla YouTube haijaingia Kenya. Umeme kule kwetu kijijini ulikuwa wazo lisilofikirika. Leo kijiji chawaka mwanga. Julia alistaafu hata kabla ya kuwepo kwa 4G. Lakini sasa ameamua kurudi ili kuwachekesha watu kwenye filamu ya Ticket to Paradise pamoja na George Clooney.
CRAIG DANIEL
Astaafu: 2015
Arejea: 2019
Baada ya filamu ya James Bond Spectre kutoka 2015, Craig aliulizwa kama ataigiza tena kama James Bond na kusema hana mipango hiyo. Alistaafu kabla ya kurejea tena mwaka uliofuata.
Baada ya filamu ya No Time To Die, 2019, akatangaza kustaafu tena. Kwa sasa anasema anataka kujikita zaidi na utayarishaji wa filamu shughuli atakayoipiga nyuma ya pazia.
JAY Z
Astaafu: 2003
Arejea: 2006
Hata kabla hajawa bilionea aliye kwa sasa, Jay Z akiwa na umri wa miaka 33, alitangaza kustaafu muziki mara tu baada ya kudondosha albamu ya The Black Anthem. Kipindi hicho alidai kuboeka na kuendelea kufanya muziki. Lakini 2006, alirejea na albamu mpya Kingdom Come na mpaka leo hii anafanya muziki kwa kujisikia.
EMMA WATSON
Astaafu: 2006
Arejea: 2010
Staa huyu wa Harry Potter alitangaza kustaafu 2007 akiwa na umri wa miaka 17 tu. Kufikia 2007 alikuwa tayari amehusika kwenye filamu tano kubwa zilizofanya vizuri.
“Nina pesa za kutosha za kula hadi nife,” alijigamba kipindi hicho. Filamu ya mwisho ya Harry Potter ilitoka 2010. Alikaa kimya kidogo kabla ya kurejea kwa kishindo akishiriki kwenye filamu kadhaa kubwa kama The Circle and The Beauty and The Beast.
ALEC BALDWIN
Astaafu: 2014
Sababu zake za kustaafu 2014 ni mapaparazzi waliokuwa wakimfuatilia sana kutokana na kuwa nyota yake ilikuwa iking’aa sana. Hakufurahia hicho na akaamua kustaafu. Lakini haikumchukua muda kabla yake kuhusika kwenye filamu zingine kubwa kama Mission: Impossible na Rogue Nation.