• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 3:16 PM
KING’ORI: Shule za mashinani pia zilindwe dhidi ya corona

KING’ORI: Shule za mashinani pia zilindwe dhidi ya corona

Na KINYUA BIN KING’ORI

Wiki Jana, shule za msingi na sekondari kote nchini zilifunguliwa baada ya kufungwa kwa miezi tisa na wanafunzi kwa sasa wamo madarasani wakiendelea na masomo japo walimu wameanza kukumbana na matatizo mengi.

Waziri wa Elimu, Prof George magoha anapaswa kuhakikisha walimu na wanafunzi wanakingwa dhidi ya maambukizi ya homa hatari ya Corona.

Shule nyingi za umma zimeshindwa kuzingatia sheria zilizowekwa na wizara ya Afya na kuwalazimu walimu wakuu wa baadhi ya shule hizo kujibunia mbinu zao wenyewe kuwashughulikia wanafunzi kutegemea na idadi yao ikizingatiwa shule nyingi hazina madarasaa ya kutosha hadi sasa.

Kwa mfano, baadhi ya wanafunzi hasa wa shule za msingi wanabadilishana barakoa bila kujali maambukizi ya homa hatari ya corona. Serikali imefungua shule lakini ukweli mchungu ni kwamba haijakuwa na mipango kabambe kuzua homa hiyo hatari.

Wizara ya Elimu isambaze sanitaiza na sabuni shuleni sawia barakoa na ielekeze jinsi zitakavyowafikia wanafunzi wote hasa maeneo ya mashambani.

Tusije kusahau kuna shule zingine hazipati maji ya mifereji yanayotiririka kila wakati ikizingatiwa lazima wanafunzi na walimu wazingatie sheria za wizara ya Afya ya kunawa mikono kwa maji inayotiririka ili kuzuia kuenea kwa Corona.

Je, wanafunzi wa shule za msingi ya Kilera na Linjoka, wadi ya Ntunene, igembe kaskazini watafuata kanuni hizo kivipi wakati ambapo kupata maji ya mifereji hata manyumbani mwao ni kitendawili?

Aidha, baadhi ya shule zinaendelea kukumbana na changamoto kubwa kutokana idadi kubwa ya wanafunzi wapya, shule za umma hasa maeneo ya mashambani zimekosa nafasi zaidi kuwaruhusu watoto ambao wazazi wao walirejea vijijini kutokana na athari ya Janga la corona, tuliambiwa na waziri wa Elimu kutakuwa na nafasi toshelezi kwa watoto wote lakini hakuna madarasaa mapya yamejengwa katika shule nyingi za umma wala madawati.

Je, ikiwa watoto wamejazana darasani watarajia walimu wabuni mbinu zipi kuhakikisha usalama wao na wanafunzi wakati huu wa covid 19 umehakikishwa?

Serikali inafaa kutoa fedha za ujenzi wa madarasa kwa shule zote za umma na ununuzi wa madawati mengine. wazazi hawawezi kukubali afya ya watoto wao ifanyiwe mzaha, japo wengi wametii amri ya kuwarejesha watoto shuleni hawakufanya hivyo kwa kupendezwa na mazingira ya shule bali wengi wanataka wana wao hasa wa darasa la nane na kidato cha nne wafanye mitihani yao ya kitaifa.

Walimu wakuu ikiwa watakosa usaidizi ufaao kutoka kwa serikali huenda wakalazimika kuwaongezea wazazi mzigo zaidi kwa kuwazidishia karo ili waweze kujenga madarasa zaidi. Ikiwa hivyo, baadhi ya walimu watatumia mbinu hiyo kuwapunja wazazi ambao hata pesa za kulipa karo kuzipata ni muujiza ya Musa kutokana na hali ngumu ya uchumi.

Nimebaini, shughuli za kuimarisha shule za umma huenda zikachukua muda mrefu kwa sababu serikali inategemea wabunge watumie fedha za NG-CDF kujenga madarasa zaidi katika maeneo yao.

Wizara ya Elimu inapaswa kukubali ukweli kwamba pesa hizo haziwezi kutosha kusaidia kufanikisha uboreshaji wa shule maadamu, zinazotengewa miundomsingi shuleni huwa asilimia ndogo huku zingine zikitumika kwa basari, usalama na maendeleo mengine katika kustawisha maeneobunge.

Waziri wa Elimu, Prof George magoha, awajibikie usalama wa wanafunzi na walimu, la sivyo, huenda shule zikafungwa tena kabla ya muhula huu kukamilika ikiwa maambukizi ya Corona yatasambaa shuleni.

You can share this post!

CHARLES WASONGA: Ni aibu sana Rais na Naibu wake wake...

WALLAH BIN WALLAH: Usitumie nguvu za kifua unapofanya kazi,...