• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
KINYUA BIN KING’ORI: Vita dhidi ya jinamizi la ufisadi viendeshwe bila ubaguzi

KINYUA BIN KING’ORI: Vita dhidi ya jinamizi la ufisadi viendeshwe bila ubaguzi

Na KINYUA BIN KINGORI

JUHUDI za kuhakikisha taifa limefanikiwa kupiga vita ufisadi lazima ziendeshwe kuambatana na Katiba, bila njama fiche na maonevu.

Itakuwa kosa ikiwa serikali itakuwa ikitumia ufisadi kufanikisha njama za kisiasa kwa nia ya kuzima baadhi ya wanasiasa kuwania nyadhifa mbalimbali katika Uchaguzi mkuu wa 2022.

Wabunge wetu wamekuwa wanafiki kiasi cha kutumiwa na viongozi wa vyama vyao kupitisha sheria zinazokinzana na katiba bila kuhamasisha raia waliowachagua umuhumu wa miswada wanayounga mkono, kupendekeza au kupitisha bila kujifahamisha ufaafu wake kwa taifa.

Kwa sasa kuna miswada miwili ya marekebisho ya sheria za madili na uongozi bora na uchaguzi inayofadhiliwa Bungeni na mwenyekiti wa kamati ya Bunge ya uhasibu wa pesa za umma (PAC), Bw Opiyo Wandanyi aliye pia mbunge wa Ugunja ambayo ikiwa itapitishwa bila marekebisho na majadiliano zaidi Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) itakuwa na mamlaka kuwazuia washukiwa wa ufisadi kugombea nyadhifa za kisiasa hasa katika uchaguzi ujao.

Je, itakuwa haki mtu kuzuiliwa kuwania udiwani hadi urais kwa kisingizio cha kutuhumiwa tu kuhusika katika ufisadi?

Je, kukabiliwa na kesi yoyote mahakamani yaweza kuwa sababu tosha kwa mtu kukosa kuidhinishwa na IEBC kugombea wadhifa wa kisiasa bila kwenda kortini kupinga uamuzi huo?

Tumeona tayari baadhi ya viongozi wa mrengo mmoja wakihangaishwa ,kushikwa na kushtakiwa kwa tuhuma za ufisadi.

Vita dhidi ya ufisadi havipaswi kuingizwa siasa, upendeleo au maonevu.

Ukweli ni kwamba baadhi ya kesi hizo huenda hazina ushahidi ila kufanikisha tu ubabe wa kisiasa.

Niambie itakuwa haki kivipi ikiwa mtu kama huyo atapigwa marufuku kuwa mgombezi wa wadhifa wowote ule kwa madai ya ufisadi na baadaye kesi yake itupwe kortini kwa ukosefu wa ushahidi toshelezi.

Katiba ya 2010 Kifungu cha 50 Ibara ya 2(a) kinasema: kila mshtakiwa ana haki ya kesi yake kusikilizwa kwa njia ya haki, ikiwemo haki ya kuaminiwa kutokuwa na hatia hadi ithibitishwe kinyume.

Hivyo, hata watuhumiwa wa ufisadi watakuwa na haki kuwania nyadhifa za kisiasa hadi kesi zao ziamuliwe, na ikiwa watapatikana na hatia watalazimika kujiuzulu nyadhifa zao.

Miongoni mwa waliopatikana na hatia ni mbunge wa sirisia John Waluke, Grace Wakhungu, Hassan Wario na wengineo.

Wanafaa kuwa wa kwanza kuzimwa kuwa wagombezi.

Wabunge wakiongozwa na Bw Wandayi wakome kujifanya malaika leo wakipitisha sheria inayoenda kinyume na katiba na kesho ya Mungu mambo yakiwabadilikia utawasikia magazetini wakilalamika na kulaumu serikali kwa kuwahangaisha.

Hatufai kukubali Bunge letu kutumiwa vibaya kupitisha sheria ambazo zitatupiliwa mbali na mahakama kama mswada wa BBI kwa kukiuka katiba yetu.

Ni kweli wafisadi hawafai kupewa nafasi kushikilia nyadhifa za umma iwe kupitia njia ya kuteuliwa au kuchaguliwa, lakini hilo kufaulu ni kupitia kuunda sheria inayoafiki hitaji la katiba na njia nyingine bora ni wananchi kuwakataa mashinani.

Mswada wa Wandayi ufanyiwe marekebisho ili uzingatie sheria na kuipa meno ya kung’ata viongozi wasiotii sheria za madili na uongozi bora.

Vita vya kupambana na ufisadi vitafaulu ikiwa serikali itaacha siasa za 2022 na kuwazuia wanasiasa wengine kuwa wagombezi kutaponza juhudi hizo zaidi na hata kuzua machafuko nchini.

You can share this post!

Marefa wa kike kusimamia mechi ya wanasoka wa kiume kutoka...

MAWAIDHA YA KIISLAMU: Baadhi ya njia ambazo Mu’umin...