• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 3:46 PM
Pasta Ng’ang’a wa Kanisa la Neno ashangaza kwa kuuzia waumini karatasi za kitabu

Pasta Ng’ang’a wa Kanisa la Neno ashangaza kwa kuuzia waumini karatasi za kitabu

NA SAMMY WAWERU

MHUBIRI tata James Ng’ang’a wa Kanisa la Neno Evangelism Centre, Nairobi ameshangaza kwa kuuzia washirika wake karatasi za kitabu.

Kwenye video, pasta huyo anaonekana akitoa karatasi kadhaa kwenye daftari kisha anazirarua kuwa vipandevipande na kuzigeuza hela.

Kwanza, katika video hiyo ya dakika mbili na sekunde kumi na tisa (2:19), Bw Ng’anga anahubiri miujiza – kupaa kwa kutumia ndege.

Naenda kutembea, niko ndani ya ndege, niko ndani ya ndege,” anasema.

Anarusha maneno mazito, “sitaki mambo ya ujinga mimi”, halafu anageukia daftari alilopakata.

Anatoa vipande vya karatasi, anaanza kushawishi waumini wake kuhusu hatua ya kuviuza.

Anazirarua vipande vidogo vidogo.

“Ukifika nyumbani kwako upasue karatasi hivi, unaskia? Unaskia ujinga wangu. Hiyo naita ni ujinga. Upasue karatasi…Sema ni pesa,” anaelezea.

La kushangaza zaidi, wafuasi wake wanajibu wakikiri karatasi hizo ni “pesa”.

Anazihesabu moja baada ya nyingine, kisha anasema; “Hiyo imefika. Hiyo ni milioni moja (akimaanisha Sh1 milioni). Haleluhya, Mungu wangu ni mkuu…Ngoja hii ninauza, ninauza mia ngapi kamoja, uende nayo?”

Anayofanya, yanafuatwa na kicheko.

Washirika wake wanamzingira, wakitoa pesa kununua vipande vya karatasi alivyorarua.

“Leta pesa, leta. Utanunua ngapi? Leta nikuuzie hii. Ndio kesho wanishambulie,” anasema akipokea pesa.

Anataja kiwango wanachonunua Sh200 na Sh500, kila kipande cha karatasi.

Aidha, anahimiza wafuasi wake kuenda na karatasi hizo waweke kwao na waandike tarehe.

“Enda uweke hii…Andika tarehe hapo. Achana na stori za watu. Ninauza karatasi,” anaelekeza.

Pasta huyo tata si mara ya kwanza amenukuliwa akihadaa waumini wake kwa ahadi za uongo.

Huku akiaminika kuhubiri kutoa mapepo, miezi kadha iliyopita video ya akishambulia washirika wake kwa kutoa sadaka kidogo ilifichuka na kusambaa mitandaoni.

Mchungaji Ng’ang’a alisisitiza kwamba matoleo ya Sh500 kamwe hayawezi kumnunulia chochote.

Kisa kingine, ni cha kujigamba kuhusu gari lake la kifahari akisema hawezi akaliendeshea barabara ya Luthuli Nairobi.

Alisuta barabara hiyo, akidai imejaa wahuni na matapeli.

Isitoshe, mhubiri huyo ameanikwa akimzaba kofi mmoja wa washirika wake alipompata akisinzia wakati wa mahubiri.

 

 

  • Tags

You can share this post!

Mashabiki wa Karen Nyamu mitandaoni wafurahia kumuona...

Miili ya maafisa 2 wa KRA walioangamizwa na El – Neno...

T L