• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 3:46 PM
PAUKWA: Bikizee akumbana na kudura ya Mungu

PAUKWA: Bikizee akumbana na kudura ya Mungu

NA ENOCK NYARIKI

KABLA ya kumkabidhi Saida zawadi yake, Bwana Mikota alitoa hotuba fupi iliyojaa majisifu na kiburi.

Maneno yake yalikuwa na nia ya kupitisha ujumbe kwa wafanyakazi wake kwamba isingekuwa wema wake kwao, maisha yao yangekuwa ya taabu tupu.

Wote walinyamaza jii na kuumeza ukweli huo jinsi mgonjwa anavyomeza mshubiri mani ilimradi apone.

“Bi Saida, wewe ndiwe mfanyakazi pekee aliyewahi kuutambua wema niliowafanyia wengi wenu. Jungu hili ni ishara ya shukrani zangu kwa uaminifu wako kazini. Hutaijutia zawadi yako maadamu jungu kuu halikosi ukoko!”

Umati ulishangilia kwa nderemo, vigelegele na vicheko mwanamke yule alipokuwa akikabidhiwa jungu lake.

Bikizee Ngima naye alipewa vyombo vya jikoni huku Mikota akimwachisha kazi kwa maneno yaliyojaa shukrani za punda: “Ngima, angalau wewe una Mungu utakayemtegemea baada ya kustaafu!’’

Wafanyakazi nao waliandaa hafla fupi ya kumuaga Bikizee Ngima. Wangempeza sana na kuukosa ushauri wake kuhusu kumcha Mungu. Saida alibadilishana zawadi yake na bikizee yule.

Alimkabidhi jungu lililojaa unga naye ajuza akamkabidhi vyombo vya jikoni.

“Mungu akifunga tundu moja la riziki hufungua mengine,’’ Bikizee Ngima aliwaaga wenzake na kuondokaJioni, alilichukua jungu lake ili akapakue unga kidogo wa kuandaa sima.

Alipoutumbukiza mkono junguni, ulikumbana na mabunda ya noti yaliyofunikwa unga! Tukio lile lilibaki kuwa siri yake jinsi zawadi ya jungu kuu ilivyokuwa siri kwa wafanyakazi wenzake.

“Wajuku wangu, mcha Mungu si mtovu!’’ Bibi Nyakebagendi alihitimisha.

  • Tags

You can share this post!

Shofco Mathare yaota mizizi ikilenga kupanda daraja

Raila Odinga amteua Martha Karua awe mgombea mwenza wake

T L