• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 5:50 AM
TAHARIRI: Hakuna raha tena kushabikia Stars

TAHARIRI: Hakuna raha tena kushabikia Stars

KITENGO CHA UHARIRI

KWA mara nyingine timu ya taifa Harambee Stars ililambishwa sakafu katika mechi ya kimataifa, raundi hii kichapo kikitolewa na Mali nchini Morocco.

Kipa Ian Otieno alitolewa kijasho kuanzia dakika ya nane Mali walipofunga bao la kwanza.

Mtindo ukawa ni kutoa ndani bao baada ya kila dakika 10 katika kipindi cha kwanza.

Kufikia mapumziko tulikuwa tumeoshwa mabao manne.

Mali walipunguza makali yao kipindi cha pili, lakini hata kwa hilo hatukufanikiwa kufunga bao la kufutia machozi.

Kufuatia kichapo hicho, Kenya sasa imeshuka hadi nafasi ya tatu kundini tukiwa na alama mbili pekee.

Stars watawakaribisha tena wapinzani wao kwa mechi ya marudiano siku ya Jumapili kuanzia saa kumi jioni.

Masaibu ya Stars yanatarajiwa kuongezeka zaidi Jumapili watakapowakaribisha tena wapinzani hao kwa mechi ya marudiano, ugani Nyayo kuanzia saa kumi jioni.

Bado vichapo vingine vinanukia mikononi mwa wenzetu wa Kundi E – Uganda, ambao siku hizi tumekuwa mboga kwao hamna tena ushindani wa zamani tuliokuwa tukiwapa.

Kwa mwelekeo huu, hata Rwanda – wanaoshikilia nafasi ya mwisho kundini – watatulambisha sakafu.

Kikosi cha akina dada wasiozidi umri wa miaka 20 jana Ijumaa pia kilibanduliwa nje ya michuano ya kufuzu kwa Kombe la Dunia 2022 nchini Costa Rica.

Hii inafuatia kichapo cha jumla cha mabao 10-3 dhidi ya Uganda.

Ni masaibu ya kusikitisha kwa wapenzi wa soka nchini, na yameletwa hususan na masihara ya Rais wa Shirikisho la soka Nchini (FKF), Nick Mwendwa.

Udikteta, ubadhirifu wa fedha rasilimali, ukosefu wa mikakati ya kukuza soka mashinani na usimamizi duni wa timu ya taifa umekuwa wimbo tangu Mwendwa achukue hatamu za kusimamia soka nchini.

Hata kwa hayo, kinara huyu haoni cha kumfanya ajiondoe kwa hiari.

Mashabiki mitandaoni tayari wameanza kujikusanya pamoja na wapenzi wengine wa soka nchini, kumtia presha Mwendwa aondoke.

Itakuwa vyema akikunja jamvi mwenyewe la sivyo shinikizo zitamuondoa.

You can share this post!

Tahadhari yatolewa kuhusu vifaa ghushi vya kupima Ukimwi

KAMAU: Kenya iziige nchi nyingine duniani kulinda tamaduni...