• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 1:01 PM
TAHARIRI: Mauaji ya vijana yatia hofu

TAHARIRI: Mauaji ya vijana yatia hofu

KITENGO CHA UHARIRI

KWA muda wa wiki mbili, vijana sita wameuawa kwa njia ya kutatanisha kwenye visa tofauti nchini na kuibua hofu kwamba vijana wa nchi hii wako kwenye hatari kubwa.

Familia mbili zimeongezwa katika orodha ya zile zinazopokonywa vijana waliokuwa na matumaini makubwa kwao na hata kwa nchi.

Kaka wawili waliouawa baada ya kukamatwa na maafisa wa polisi katika kijiji cha Kianjakoma, kaunti ya Embu kwa kukiuka kafyu walikuwa wanafunzi wa vyuo vikuu. Naam, familia ilipokonywa wavulana wawili iliyotumia nguvu, kujinyima na rasilmali ili kuwapa elimu bora.

Ingawa uchunguzi kuhusu jinsi wawili hao walivyokufa unaendelea, polisi hawawezi kuepuka kidole cha lawama.

Kabla ya Wakenya kusahau mauaji ya vijana hao, familia nyingine eneo la Syokimau inaomboleza baada ya vijana wawili kuuawa kikatili kaunti ya Kajiado kwa madai finyu kwamba walikuwa wezi wa mifugo.

Kulingana na polisi, hakukuwa na mifugo walioibwa eneo hilo wakati huo na isitoshe, vijana hao walikuwa na pikipiki ambazo haziwezi kubeba ng’ombe.

Vijana wa mama mmoja, ambao walikuwa wakisherehekea siku ya kuzaliwa ya rafiki yao. Kwamba vijana hao walioondoka katika nyumba yao ya kifahari waliuawa kwa kushukiwa kuwa wezi wa mifugo katika eneo lililo na maafisa wa usalama na utawala ni jambo la kuatua moyo.

Visa hivi na vingine vya vijana kutekwa na kutoweka, kuuawa kwa kupigwa risasi kiholela na maafisa wa polisi kwa kudaiwa kuhusika na uhalifu bila ushahidi vinatoa mwelekeo hasi kwa jamii tunayoishi. Mwelekeo ambao ni hatari kwa usalama wa taifa na jamii kwa jumula.

Vijana, ambao ni tegemeo la nchi siku zijazo wakiangamizwa na maafisa wa polisi wanaofaa kuwalinda ni ishara ya nchi isiyojali ustawi wake.

Ni sawa na kukatiza siku zijazo za nchi. Ni mtindo unaofaa kuzimwa. Awali ilikuwa ni vijana kutoka mitaa ya mabanda inayoishi watu masikini waliouawa na polisi kwa kushukiwa kuhusika na uhalifu lakini sasa, hali imebadilika hivi kwamba hata wale wa matabaka ya juu, walio na taaluma zao wanauawa na polisi.

Hii inawafanya vijana kuwachukulia maafisa wa usalama kuwa maadui. Maafisa wa polisi wanafaa kufahamu kuwa vijana wanaoua kiholela ni sawa na watoto na ndugu zao.

You can share this post!

Jagina wa soka kambini mwa Bayern na Ujerumani, Gerd Muller...

TSC yashtakiwa kukata ada walimu wasio vyamani