• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 1:14 PM
TAHARIRI: Vijana wapewe vitambulisho upesi

TAHARIRI: Vijana wapewe vitambulisho upesi

KITENGO CHA UHARIRI

SHUGHULI ya usajili wa wapigakura kitaifa ilianza jana ambapo Tume ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) inalenga kusajili zaidi ya Wakenya milioni nne.

Usajili huo ukifanikiwa, Kenya itakuwa na jumla ya angaa wapigakura milioni 24 bila kuzingatia awamu nyingine ya usajili inayotarajiwa kufanyika Januari 2022.

Je, idadi hiyo itafikiwaje bila kuwawezesha vijana ambao ndio wengi wanaolengwa katika usajili huu?

Zaidi ya asilimia 90 ya wanaotazamiwa kusajiliwa ni vijana.

Changamoto kuu ambayo imejitokeza kuhusu kufaulisha azimio la kusajili angaa wapigakura milioni nne wanaolengwa mwezi huu wa Oktoba ni ukosefu wa vitambulisho.

Hii ni kwa sababu shughuli ya vijana kupewa vitambulisho imeanza siku chache zilizopita, hali inayomaanisha kuwa haitakuwa rahisi kusajiliwa kama wapigakura katika usajili wa mwezi huu kwa sababu shughuli hizo zote mbili zinaenda sambamba.

Vitambulisho huchukua angaa mwezi mmoja kabla ya kuwa tayari kuchuliwa na waliotuma maombi ya kupewa.

Katika muda huo wa kusubiri, vijana hupewa stakabadhi ya kuonesha kuwa wanangoja kupewa vitambulisho kamili.

Haieleweki ni sababu gani serikali, katika enzi hii ya kidijitali bado inajikokota katika kutoa huduma muhimu kwa wananchi kama vile kuwapa vijana na raia wake vitambulisho.

Wengi wao wanaoshika vitambulisho sasa wataweza tu kujisajili kama wapigakura kwenye mkumbo wa Januari.

Maadamu IEBC imelenga jumla ya wapigakura milioni saba katika mikumbo hii miwili ya usajili, basi itakuwa vigumu kufikisha idadi hiyo iwapo wengi hawatapata vitambulisho hivi kwa sasa ndipo wajisajili.

Inapozingatiwa kuwa upigaji kura ni haki ya kidemokrasia ya kila Mkenya, iwapo vijana hao hawatakuwa wamepata vitambulisho vya kuwawezesha kujisajili kwa madhumuni hayo, basi watakuwa wamenyimwa haki yao; jambo ambalo si zuri.

Mbali na vijana, IEBC inahitajika kujitahidi kuhakikisha kuwa shughuli nzima ya usajili wa wapigakura imeendeshwa vyema bila hila zozote zinazoweza kutokea.

Kwa mfano, wapo baadhi ya watu ambao tayari wameanza kulalamika kuwa kuna wanasiasa fulani ambao wameanza kuhamisha wapigakura kutoka maeneo wanakostahili hadi kwenye maeneo yao kwa nia ya kujipa ushindi katika uchaguzi wa 2022.

Sharti njama kama hizo zizimwe.

You can share this post!

PATA USHAURI WA DKT FLO: Kwa nini mjamzito huvuja damu...

Wanasiasa wabuni njama IEBC ikisajili wapigakura wapya