NA RICHARD MAOSI
MCHEZO wa sarakasi na kwata ya watoto unatambulika tangu zamani kutokana na ufaafu wake katika kuupa mwili nguvu kwani kupitia uzoefu ndipo ujuzi wake hupatikana.
Kwa ndugu wawili Malvin Cheruiyot, 11, na mwenzake Elvis Kipkoech, 13, wote wakiwa wanafunzi katika shule ya msingi ya Baharini Nakuru, kufanya mazoezi ya mara kwa mara ndio siri ya kufanikiwa katika mchezo huu.
Kwa mujibu wa Malvin ambaye yuko katika darasa la saba, wao hufanya mazoezi kila siku ya Jumamosi na Jumapili, lakini inapofika likizo wao hufanya mazoezi ya kila siku.
Anasema yeye na kaka yake walianza kujifunza mchezo wa sarakasi mwaka wa 2021, baada ya shule zote nchini kufungwa kwa muda mrefu kutokana na chamko la homa ya corona.
“Tulikuwa na muda mwingi wa kukaa nyumbani ndiposa tukaona haja ya kujiunga na kikundi kimoja huku mtaani kujifundisha sarakasi,” akasema.
Anasema kwa mara ya kwanza walipata ugumu lakini baadaye walijizatiti mpaka wakafanikiwa na kupata ujuzi wa kusimama wima juu ya bega la mwenzake, ikizingatiwa kuwa kinachohitajika ni udhabiti wa mwili.
Aongeza kuwa ili kuwa mchezaji bora wa sarakasi ya watoto, unahitaji kuwa makini, kuwa na subira, kujiamini na kutia bidii kabla ya kubobea katika tasnia hii.
Kulingana naye, sarakasi ya watoto huwasaidia kuweka miili yao katika hali nzuri na kukuwa jasiri wanapoonyesha ujuzi wao mbele ya hadhira.
Kwa upande mwingine, Elvis anasema kuwa wazazi wao wamekuwa nguzo muhimu kwa mafanikio yao kwa sababu wamekuwa wakiwanunulia sare rasmi za kufanya mazoezi, mbali na kuwalipia nauli wakati wa kushiriki tamasha za hadhi ya juu ndani na nje ya kaunti ya Nakuru.
Isitoshe, anaongeza kuwa wamekuwa wakitumbuiza wageni katika Sherehe za Kitaifa kama vile siku ya Jamhuri katika uwanja wa Afraha.
Anaomba serikali za kaunti na zile za kitaifa kuanzisha taasisi maalum za kufundisha mchezo huu ili kutambua talanta nyingi mashinani, hali ambayo itawasaidia vijana kujiajiri na kuwaajiri wengine.
Lengo lao kuu ni waje kuwa watumbuizaji kwenye kiwango cha kimataifa, ili wapate fursa ya kuzuru mataifa ya Ulaya.
Subscribe our newsletter to stay updated